Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora

Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora
----------------------WE THANK AND APPRECIATE YOU FOR VISITING CHADEMA DIASPORA BLOG. AGAIN, THANK YOU!-----------------------

Thursday, January 16, 2014

Ni Mazoea ya Hatari kuacha Kamati Kuu(CCM) Iwaite na Kuwahoji Mawaziri - Itatuletea Matatizo Mbeleni

NI MAKOSA NA HATARI KUACHA KAMATI KUU YA CHAMA KUWAHOJI NA KUWAPIMA MAWAZIRI


Na. M. M. Mwanakijiji

Kuna jambo la hatari limetokea nchini jambo ambalo tumelikubali na kuona kuwa ni halali. Jambo hili litakuwa na matokeo na yawezekana tayari limekuwa na matokeo katika utendaji kazi wa serikali pale ambapo wanasiasa wanapoamua kuamua hatima ya watendaji wa serikali na hata kuingilia kati utendaji wa serikali katika mfumo ambao haupo katika Katiba na Sheria zetu.

Tatizo hili ni kubwa sana na inashangaza siyo wanasiasa wetu (wa chama tawala au upinzani) na wala siyo wasomi wetu (wa Katiba na wengine) ambao wamesimama kulionesha tatizo hili na hatari yake katika kutengeneza mfumo mzuri wa utawala wa sheria katika nchi ya kidemokrasia. Ni vizuri nifafanue jambo hili ili wasomaji wangu waelewe kuwa kukubali Kamati Kuu ya chama cha siasa kuingilia wajibu wa Rais ambao ni wa kwake peke yake (presidential prerogative) ni jambo la kupinga, kukejeli na kulikataa kwa lugha kali inayowezekana. Kwanini?

1. Wakati Rais anateua Mawaziri Hakuomba Maoni toka Kamati Kuu ya Chama chake

Katika ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeweka uteuzi wa mawaziri kama miongoni mwa yale majukumu ya kipekee ya Rais (presidential prerogatives) ambayo hawezi kuingiliwa na mtu yeyote katika kutekeleza. Majukumu mengine ya aina hii ni kama kusamehe wafungwa, kufuta adhabu ya kifo na kutangaza vita.

Ibara ya 55 ya Katiba inasema kuwa Rais anaweza kuwateua Mawaziri na Manaibu Waziri kwa idadi yoyote ile baada ya kushauriana na Waziri Mkuu. Katiba haisemi kuwa Rais anapaswa kufuata ushauri huo wa Waziri Mkuu ndio maana katika Ibara ya 58 inasemwa “Mawaziri na Naibu Mawaziri watashika madaraka yao kwa ridhaa ya Rais, na watalipwa mshahara, posho na malipo mengineyo kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge.”

Hii ina maana moja tu; Mawaziri hawafanyi kazi na hawawajibiki kwa namna yoyote mbele ya Kamati Kuu ya Chama chao. Wanawajibika mbele ya Rais peke yake. Kitu kinachotupa sababu ya pili.

2. Rais peke yake ndiyo anawajibu wa kuhoji utendaji kazi wa mawaziri na manaibu waziri wake

Hili ni jambo linalotokana na hilo hapo juu. Kama Mawaziri wanateuliwa na Rais na kama wanafanya kazi kwa ridhaa yake (at his pleasure) basi ni yeye peke anayeweza kuhojiwa juu ya utendaji wao. Kuwaita Wateule wa Rais “mizigo” ni kumuita mteuaji “mbeba mizigo”. Huwezi kuwasema walioteuliwa tena ukawananga vilivyo na wakati huo huo ukawa unaheshimu aliyewateua!

Kama walioteuliwa wanaboronga, na aliyewateua hawawajibishi hadi watu walalamike au hafuatilii utendaji wao kwa karibu kiasi kwamba wanaonekana kuwa mizigo kwa chama chake basi mwenye kubeba wajibu huo ni yeye mteuaji. Wamarekani wanamsemo kuwa “the bucks stops with the president” kwa maana ya kwamba mambo yote mwisho wake mwenye kuwajibika ni Rais. Hivyo, Kamati Kuu ya chama haiwezi kufanya kazi ya Rais, haipaswi kufanya kazi ya Rais na ni makosa kuiacha idhanie kuwa inaweza kumsaidia Rais kusimamia Mawaziri! Kitu ambacho kinatupa sababu ya tatu ya kwanini jambo hili ni la hatari na la kukatiliwa vikali.

3. Katiba ya CCM haitoi mamlaka kwa Kamati Kuu ya CCM kuwasimamia Mawaziri wa serikali

Ibara ya 109 ya Katiba ya CCM imeweka bayana kazi na majukumu ya Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM. Kazi zake zote ni za kisiasa na zinahusiana na utendaji kazi wa chama na si wa serikali. Hii ina maana Kamati Kuu ya CCM haina madaraka yoyote ya kuwaita, kuwahoji au kuwapa maelekezo ya kiutendaji wateule wa rais wa ngazi yoyote ile; siyo mawaziri, siyo manaibu, wala siyo wakuu wa mikoa! Madaraka hayo haina na haijapewa na hivyo kimsingi ni kuingilia kazi za vyombo vingine. Hili linatupa jambo la nne.

4. Ibara ya 63 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano imetoa nafasi kwa mawaziri wa serikali kuulizwa juu ya wizara zao na utendaji wao wa kazi. Kifungu kidogo cha 3(a) cha Ibara hiyo kinasema kuwa Bunge laweza “kumuuliza Waziri yeyote swali lolote kuhusu mambo ya Umma katika

Jamhuri ya Muungano ambayo yako katika wajibu wake;” Hili linajibu swali jepesi tu; sasa kama Kamati Kuu ya chama haiwezi kuwauliza mawaziri nani basi ukimuondoa Rais anayeweza kuwauliza maswali na kuwawajibisha mawaziri? Jibu liko katika Ibara hiyo na ibara nyingine ambayo imelipa Bunge uwezo wa kupiga ya kutokuwa na imani na serikali (ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu).

Kama kuna kiongozi au mwanachama yeyote ndani ya CCM ambaye hafurahii utendaji kazi wa waziri yeyote njia pekee na rahisi ya kumfuatilia waziri au kuwafuatilia mawaziri hao ni kupitia wabunge wa chama hicho Bungeni. Hili ni muhimu hasa ukizingatia ukweli kuwa CCM ina wabunge wengi zaidi kiasi cha kwamba hawahitaji kura za upinzani kupitisha jambo lolote Bungeni (wana wingi wa theluthi zaidi ya mbili). Hivyo, kama kuna waziri mzigo njia na mahali pekee pa mawaziri hao kuhojiwa na kuwajibishwa ni Bungeni na hilo linaweza kufanywa na wabunge tu.

Na kama wabunge wa CCM wanaona serikali yenyewe ndio tatizo wana njia nyingine mbili za kuiwajibisha; kupiga kura ya kutokuwa na imani na Rais au kutafuta sababu ya Kikatiba ya kumuondoa Rais Madarakani kupitia Mashtaka ya Kibunge (Impeachment).

Kufuatia kutangazwa kwa Baraza Jipya la Mawaziri hoja hizi hapa ni muhimu kuzingalia na kuzizingatia kwani kama tutaacha huu “mchezo” wa kisiasa ambapo chama cha siasa kinaingilia majukumu ya Rais hatutakuwa na serikali iliyo thabiti (stable) madarakani kwani itakuwa serikali ambayo badala ya kufanya kazi kwa ridhaa ya Rais inafanya kazi kwa ridhaa ya Kamati Kuu ya chama.

Ni kwa sababu hiyo kwa madaraka yangu ya kipekee niliyojipatia mimi mwenyewe; nikizingatia dhamira yangu natangaza na kuwataka mawaziri wote wapya na wale wazamani kukataa mara moja kusimama mbele ya Kamati Kuu ya chama kutoa maelezo yoyote isipokuwa Bungeni au mbele ya Rais. Hii si kwa ajili ya utukufu wao bali kwa ajili ya kutenganisha wazi kabisa majukumu ya vyombo mbalimbali nchini ili kuhakikisha hakuna mwingiliano haramu.

Na kwa madaraka hayo ninawataka mawaziri wote ambao watajikuta wanalazimishwa kuweka vyeo vyao mbele ya altare ya chama chao cha siasa kuamua kujiuzulu kazi zao mara moja kuliko kujidhalilisha kama walivyojidhalilisha baadhi ya mawaziri wiki chache zilizopita ambao kwa woga wao na kukosa kwao msimamo waliitwa na kusimama mbele ya Kamati Kuu ya CCM.

Na wakati umefika kwa Rais Kikwete kuanza kukubali kuwajibika kwa makosa ya mawaziri wake haiwezekani awe anapata nafasi ya kubadilisha tu na siyo kuwafuatilia au yeye mwenyewe kuwajibika. Kwani yeye ndiye mamlaka ya juu ya uteuzi na uwajibishaji na kushindwa kwake kuwawajisha mawaziri wake hadi chama chake kiamue kumsaidia ni udhaifu mkubwa na wa hatari katika demokrasia yetu. Ni lazima awe tayari kusimama na mawaziri wake au yeye mwenyewe kuwakingia kifua kuliko kuwatosa kila wakati mambo yanapokuwa magumu na kusingizia ni “kuwajibika kisiasa”. Na sisi tungependa kuona nay eye anawajibika kisiasa kama wengine au yeye mwenyewe awawajibishe bila kulazimishwa na Bunge. Kama hana muda, nia, uwezo au uthubutu wa kufanya hivyo ni vizuri akaamua nay eye ajipime mbele ya wananchi kama anastahili kuendelea na majukumu yake au atumie haki yake chini ya Katiba ili ampishe Makamu wake kufanya kile ambacho yeye ameshindwa.

Vinginevyo, atajikuta analiachia taifa mojawapo ya mazoea (precedence) mbaya sana ya kiutawala nchini ambayo ikikubaliwa kama ilivyokubaliwa sasa serikali zetu huko mbeleni zitapata kazi sana kusimama madarakani.

Na kwa Mawaziri na Manaibu wao wapya – karibuni kazini na nyinyi mtawajibishwa pia.

Heri ya Mwaka Mpya!

Niandikie: mwanakijiji@jamiiforums.com
Nitafute Facebook: “Mimi Mwanakijiji”

Nifuate Twitter: “Mwanakijiji”

No comments: