Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora

Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora
----------------------WE THANK AND APPRECIATE YOU FOR VISITING CHADEMA DIASPORA BLOG. AGAIN, THANK YOU!-----------------------

Tuesday, September 3, 2013

'Hatutaki Rais ateue wabunge wetu'


WAJUMBE wa mdahalo wa kupitia rasimu ya Katiba mpya, wamependekeza katiba hiyo, itoe fursa kwa vyama vya watu walio na ulemavu kuchagua wawakilishi wao bungeni, badala ya wabunge hao kuteuliwa na Rais. Mapendekezo hayo yalitolewa na wajumbe hao juzi, katika mdahalo uliofanyika katika kijiji cha Milanzi wilayani Sumbawanga, ulioandaliwa na asasi ya Vijana wa Kupambana na Maendeleo Rukwa (VIPAMARU), kwa ufadhili wa The Foundation For Civil Society. Mmoja wa wajumbe hao, mwalimu Thomas Sepe, ambaye pia ni mlemavu wa macho, alisema kutokana na majukumu mengi aliyonayo Rais, ni vigumu kuwatambua walemavu walio na sifa stahiki ya kuwakilisha wenzao.
  
       Sepe aliwataja walemavu waishio maeneo ya pembezoni kuwa miongoni mwa wenye uwezo lakini ni vigumu kuteuliwa na Rais kwa kuwa ni vigumu sifa zao kumfikia. Alisema kuvipa majukumu vyama vya walemavu kuchagua wawakilishi kutatoa fursa kwa walemavu walioko pembezoni kushiriki kwenye mchakato huo na kuwezesha kupatikana kwa wawakilishi walio na sifa zinazoweza kuitetea jamii hiyo. Katika kujadili rasimu hiyo ya katiba, wajumbe wa mdahalo huo pia walilalamikia hatua ya nakala za rasimu kutokuwa na dibaji ya kumwezesha msomaji kujua jambo analohitaji linapatikana katika ukurasa upi. 

      Changamoto nyingine iliyobainishwa na wajumbe hao ni kukosekana kwa tafsiri za misamiati iliyopo katika rasimu ya katiba. Walisema hali hiyo inasababisha wasomaji kushindwa kupata maana halisi ya baadhi ya vipengele vya rasimu hiyo. Mmoja wa washiriki, Willy Nsalanga alipendekeza katiba ijayo iongeze kuwepo na siku tisini kati ya siku ya kutangazwa kwa mshindi wa urais hadi siku ya kuapishwa ili kutoa fursa kwa wanaopinga ushindi wake kuchukua hatua stahiki.

Source: Nyambo J. (Sept. 2013). 'Hatutaki Rais ateue wabunge wetu'. Sumbawanga. Retrieved from HabariLeo 

No comments: