Na Zitto Kabwe
KAMATI
za Bunge za Hesabu ni asasi muhimu za Bunge katika kuhakikisha serikali
inawajibika kwa wawakilishi wa wananchi. Majukumu ya kamati hizi yameainishwa
na Kanuni za Bunge, nyongeza ya nane. Nyaraka muhimu na ya kwanza katika kazi
za kamati za kusimamia hesabu ni ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu
za Serikali (CAG). Hivyo
Kamati za Bunge za Hesabu pamoja na CAG, wanapaswa kufanya kazi kwa ushirikiano
mkubwa. Ndiyo maana bajeti ya CAG inapitishwa na PAC na ikishapitishwa hakuna
mamlaka ya kuhoji tena. Vile vile PAC ndio Kamati yenye mamlaka ya kuteua
mkaguzi wa hesabu za ofisi ya CAG.
Ni
wajibu wa Kamati za Bunge za Hesabu kulisaidia Bunge katika kuiwajibisha
serikali. Mara kadhaa kumekuwa na maelezo kwamba kazi ya Bunge ni kuishauri
serikali, hapana. Katika kuisimamia serikali ndani yake kuna ushauri hivyo
ushauri haupaswi kuwekewa mkazo zaidi ya usimamizi. Warasimu
wa serikali wanapenda neno ushauri na kuchukia neno usimamizi. Wabunge
hawapaswi kuingia katika mtego wa ‘kazi yao ni kushauri’ kwani huo ni mtego
uliotegwa na warasimu ili kupunguza nguvu ya Bunge. Kazi ya Bunge ni kusimamia
serikali.
Kamati
za Bunge za Hesabu ndizo zenye kubeba mzigo huo mkubwa kwa niaba ya Bunge na
kwa hiyo, uadilifu ni jambo la msingi katika wajibu huu. Vile vile ndio maana
ni rahisi kuona Kamati za Hesabu zikipewa kila aina ya shutuma kutoka kwa
wasimamiwa na wakati mwingine kwa kuwatumia baadhi ya wabunge kwa kujua au
kutokujua. Wakati
mwingine Kamati za Bunge huambiwa kuangalia ‘mahesabu tu’ basi. Ni wajibu wa
Kamati za Bunge kuangalia hesabu za umma na kuona kama matumizi ya fedha za
umma yanafanikisha malengo yaliyotarajiwa (performance audit).
Itakuwa
ni wendawazimu kwa kamati kuridhika kwa kuangalia tu mizania ya serikali au
mashirika ya umma au serikali za mitaa. Kwa mfano, ni wajibu wa kamati
kuangalia kama fedha zilizotolewa kwa ujenzi wa barabara zimetumika kwa kazi
hiyo. Ni wajibu zaidi wa kamati kuangalia kama gharama hiyo iliyotumika kujenga
barabara husika ndio gharama halisi na sio kwamba imezidishwa ili kunufaisha
watu wachache. Ni
wajibu mkubwa zaidi wa kamati kuangalia kama barabara hiyo imejengwa kwa
kiwango kinachotakiwa. Hii inaitwa ‘value for money’. Katika utendaji wa kazi
hizi ni muhimu na lazima, Kamati za Bunge kutumia kwanza taarifa ya CAG. Hata
hivyo, kamati pia zinaweza kutumia taarifa kutoka vyanzo vingine mbalimbali
kama wananchi na vyombo vya habari, katika kufikia malengo ya kuchunguza.
Kwa
mfano, hivi karibuni moja ya magazeti hapa nchini yaliandika kuhusu matumizi
mabaya ya fedha katika mkutano wa Smart Partnership, kwamba takribani shilingi
bilioni nane zimefanyiwa ufisadi. CAG amenukuliwa akisema hajapata barua yoyote
inayomwomba (CAG haagizwi, anaombwa) kufanya ukaguzi maalumu wa mkutano ule. Kamati
ya Bunge ya PAC inaweza kutumia mamlaka yake kumwomba CAG kufanya ukaguzi
maalumu na kuwasilisha matokeo yake kwenye kamati na hatimaye bungeni.
Iliyokuwa Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC) ilifanya wajibu huu
vizuri kwenye suala la nyumba ya Gavana wa Benki Kuu na kutokana na ukaguzi huo
hoja ile ilifungwa.
Ili
kutekeleza wajibu huu muhimu wa uwajibikaji, Kamati za Bunge za Hesabu ni
lazima ziwezeshwe vya kutosha kwa mafunzo ya ujuzi (skills) na maarifa (knowledge).
Bila ya kuwa na uelewa mpana wa mambo kamati hujikuta zikifanya uamuzi wenye
madhara makubwa kwa taifa. Katika
kutekeleza wajibu, ni muhimu na lazima wajumbe wa kamati kujiepusha na vitendo
vya rushwa kwani vitendo hivyo huzuia usimamizi na hatimaye kuendeleza rushwa
kwa wanaosimamiwa. Uwajibikaji ni silaha dhidi ya rushwa na hivyo wanaosimaima
uwajibikaji ni lazima wawe wasafi, wao binafsi kwanza kabla ya kusafisha walio
wachafu. Uadilifu
ni msingi muhimu katika kujenga uwajibikaji. Bila ya uadilifu hakuna
uwajibikaji na vile vile kukosekana kwa uwajibikaji humomonyoa utamaduni wa
uadilifu katika jamii.
Mambo gani ya kuzingatia?
Tumeona
wajibu wa Kamati katika kusimamia uwajibikaji wa serikali. Baadhi ya mambo
muhimu ya kuzingatia ni katika utekelezaji wa wajibu huu ni; moja, pamoja na
matumizi yote ya serikali ambayo kamati husimamia, kuna matumizi ambayo inabidi
kuweka msisitizo maalumu. Kati
ya matumizi hayo ni pamoja na deni la taifa. Katika ripoti ya CAG ya mwaka
2012, hoja za kuhusu deni la taifa zimeendelea kutokana na kasi ya ongezeko
lake. Kamati inapaswa kufahamu kwamba mzigo mkubwa wa deni hilo ni katika
kulipa kwa kutumia fedha nyingi za umma. Kila
mwaka bajeti ya kuhudumia deni la taifa huwa ni moja ya bajeti kubwa zaidi ya
bajeti nyingine zote. Kwa mfano mwaka 2012/13, serikali ilitenga takribani
shilingi trilioni mbili kuhudumia deni hilo pekee ilhali robo tu ya fedha hizo
ilitengwa kwa ajili ya Wizara ya Afya.
Kamati
zinapaswa kukagua kwa kina na kila wakati matumizi ya mikopo ili kuhakikisha
inatumika kujenga uwezo wa nchi kuzalisha rasilimali za kuhudumia mikopo hiyo
kwa kukuza uchumi, kuzalisha ajira na kuongeza kodi. Pili,
makusanyo ya kodi ya serikali. Bunge hupitisha fedha kuwezesha Mamlaka ya
Mapato Tanzania (TRA) kukusanya kodi. Hivi sasa ni takriban Watanzania milioni
moja tu wanalipa kodi (kwa maana ya watu binafsi walio kwenye mfumo rasmi).
Hivyo
tuna wigo mdogo sana wa kodi wakati tunatumia fedha nyingi kukusanya kodi hiyo
kidogo. Ni wajibu wa kamati kuona kwamba ufanisi katika kukusanya kodi
unafikiwa, sambamba na kuzuia mianya ya ukwepaji wa kodi. Kwa
mujibu wa TRA, asilimia 15 ya makusanyo yanayotarajiwa huwa hayakusanywi kwenye
idara ya mapato peke yake kutokana na ukwepaji wa kodi. Hii ni sawa na
takribani shilingi bilioni 490 kwa kutumia makadirio ya mwaka wa fedha 2012/13.
Wakati
Bandari ya Dar es Salaam inapakua makontena 600 kwa zamu (shift), kuna
wakala wa upakuaji (clearing and forwarding agents) wa idadi hiyo hiyo katika
Bandari hiyo. Haiwezekani kuwe na wastani wa kontena moja kwa kila wakala. Eneo
hili linahitaji jicho pevu kutoka Kamati za Bunge na CAG. Ukwepaji
kodi wa kampuni za kimataifa pia ni ajenda kubwa ambayo kila mara kamati
inapaswa kuizingatia ili kuzuia. Kamati ya PAC tayari imepitisha mapendekezo ya
ukaguzi wa misamaha ya kodi na kuiweka wazi (audit of tax exemptions and
transparency).
Ni
matarajio kwamba kwenye ripoti ya CAG kwa mwaka unaoishia Juni 2013, Watanzania
wataona taarifa ya ukaguzi wa misamaha ya kodi. Tatu,
ukaguzi wa mikataba na taratibu za ununuzi. Hili ni eneo ambalo limekuwa chanzo
kikubwa cha ubadhirifu nchini. Ni muhimu kila mara kamati kuzingatia eneo hili
katika kazi zake. Eneo hili linaathiri zaidi mamlaka za serikali za mitaa,
udokozi umekuwa kama utamaduni na hivyo kuzorotesha utoaji wa huduma kwa
wananchi.
Ni
muhimu kamati kuhitaji mara kwa mara ukaguzi maalumu kwenye masuala ya ununuzi
ili kujenga uwajibikaji katika eneo hilo na kuepusha hasara kubwa kwa nchi. Nne,
hivi sasa nchi yetu imekuwa kitovu cha biashara ya dawa za kulevya. Vijana
wa kitanzania wamekuwa wakikamatwa maeneo mbalimbali duniani wakihusishwa na
biashara ya dawa za kulevya. Moja ya njia ya kupambana na uharamia huu ni
uwajibikaji wa mamlaka zenye wajibu wa kupambana na dawa za kulevya.
Hivyo,
Kamati za Bunge zihoji katika hesabu za mamlaka hizo matumizi ya fedha za umma
katika kupambana na biashara ya dawa za kulevya ilhali biashara hiyo inazidi
kushamiri. Iwapo
tutaiwajibisha Wizara ya Mambo ya Ndani, kitengo cha kupambana na dawa za
kulevya tutakuwa tumechangia katika vita hii. Hatuwezi kuendelea kutenga fedha
kila mwaka dhidi ya biashara hii haramu lakini bado inazidi kushamiri. Kila
mwenye wajibu awajibishwe.
Jambo
jingine ni kuhusu ukaguzi wa mchakato wa ubinafsishaji. Bado sera ya
ubinafsishaji inatekelezwa na serikali. Ni wajibu wa CAG kukagua mchakato wa
ubinafsishaji na Kamati za Bunge kusimamia uwajibikaji katika mchakato huo.
Ubinafsishaji ni uuzaji wa mali ya umma, hivyo ni lazima upate usimamizi
kamilifu. Kwa
kuhitimisha, nieleze kwamba Kamati za Bunge za Hesabu ni asasi muhimu za
demokrasia kwa sababbu husimamia uwajibikaji. Ni vema kamati hizi kupewa uzito
stahili kwa kuwa na rasilimali za kutosha katika kufanya kazi zake na
kuhakikisha taarifa zake zinapata uzito katika utekelezaji.
Kimsingi
kamati zote za Bunge ni sawa kwa hadhi lakini Kamati za Hesabu ndio Bunge kwa
uhalisia.
No comments:
Post a Comment