Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora

Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora
----------------------WE THANK AND APPRECIATE YOU FOR VISITING CHADEMA DIASPORA BLOG. AGAIN, THANK YOU!-----------------------

Monday, January 20, 2014

Mambo matatu yaitesa CCM

       
   MBIO za kusaka urais kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), na uteuzi wa nafasi nne za mawaziri, vinaelezwa kukibomoa chama hicho, Tanzania Daima limedokezwa. Mbali na mambo hayo, mchakato wa uundwaji wa katiba mpya ambayo rasimu ya pili imetoka hivi karibuni na kuingizwa kwa serikali tatu, umeonekana kukiathiri zaidi chama hicho kinachotaka uwepo wa serikali mbili. Tayari viongozi wa CCM wameshaanza maandalizi ya kukutana na wabunge, wawakilishi na wabunge wa Bunge la Katiba watakaochaguliwa, kwa lengo la kuweka msimamo wa kutopitisha serikali tatu wakati wa majadiliano. Wanataka hoja ya serikali tatu isifikishwe kwenye kura ya maoni ambako wana hofu inaweza kupata uungwaji mkono. Hofu ya makada hao wa CCM ni kuwa muundo wa serikali tatu utabomoa muungano wa Tanganyika na Zanzibar ulioasisiwa na Rais wa Kwanza wa Zanzibar, Abeid Amani Karume na Julius Nyerere aliyekuwa Rais wa Tanganyika.
       Wakati suala la katiba mpya likionekana kuwaumiza vichwa makada wa chama hicho, mbio za urais unaotarajiwa kufanyika mwakani, nazo zimezidi kukipasua chama hicho. Hadi hivi sasa viongozi wa CCM wamekuwa wakipambana na aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa ambaye katika siku za hivi karibuni alitangaza safari ya matumaini kuelekea ndoto zake za kuwapatia Watanzania elimu bure na huduma bora za msingi. Lowassa, alitangaza safari hiyo iliyotafsiriwa ni ya kuwania urais katika mkesha wa mwaka mpya jimboni kwake Monduli, ambako aliwaalika makada mbalimbali wa CCM wakiwemo wajumbe wa vikao muhimu vya maamuzi. Miongoni mwa waliokuwepo kwenye hafla hiyo ni Mwenyekiti wa wenyeviti wa chama hicho, Mgana Msindai, ambaye alisema wanaunga mkono safari ya Lowassa. Tangu Lowassa atangaze safari yake hiyo, viongozi wa CCM, akiwemo Makamu Mwenyekiti (bara), Philip Mangula, wamejitokeza hadharani kumpinga.
         Mangula alisema chama chake kimeunda timu ya kuchunguza makada wake walioanza harakati za kuwania uongozi kabla ya pazia kufunguliwa, na wakibainika kutenda kosa hawatapewa nafasi ya kuwania nafasi husika. Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), nao ulitaka Lowassa atimuliwe kwa madai ya kukivuruga chama na kupanga safu yake ya kuwania madaraka ilhali Rais Jakaya Kikwete hajamaliza muda wake. Wakati chama hicho kikionekana kupambana na Lowassa, mbunge huyo juzi katika ukusara wake wa mtandao wa kijamii wa Facebook aliandika: “Ukiona unatumia nguvu nyingi kumchafua mtu kwa kumpakazia mambo, kumsengenya, kumfitinisha na kumsingizia, ujue yeye ni bora kuliko wewe, kichafu kinaonekana hata bila kuambiwa.”
Uwaziri moto
       Nafasi nne za mawaziri waliotenguliwa uteuzi wao kutokana na kuguswa na kashfa ya vitendo vya ukiukwaji wa haki za ubinadamu katika Operesheni Tokomeza Ujangili, nazo zimewafanya makada wa chama hicho kupigana vikumbo kila kukicha. Mawaziri hao ni Khamis Kagasheki (Maliasili na Utalii), Shamsi Vuai Nahodha (Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa), Emmanuel Nchimbi (Mambo ya Ndani) na David Mathayo (Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi). Baadhi ya wabunge na mawaziri inadaiwa wamekuwa karibu na familia ya Rais Kikwete ili wapate fursa ya kuwemo kwenye baraza la mawaziri ambalo linatarajiwa kufanyiwa mabadiliko makubwa. Tanzania Daima Jumapili, limedokezwa kuwa baadhi ya wabunge na mawaziri wamekuwa wakitapeliwa na watu wanaojitambulisha ni askari wa usalama wa taifa. Inadaiwa askari hao wamekuwa wakiwaeleza mawaziri na wabunge kuwa wamepewa jukumu la kuandika ripoti au kufanya uchunguzi juu ya mienendo ya wahusika na ili waandike yaliyo bora huwadai fedha wahusika. Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue, aliwataka wabunge na mawaziri wasirubunike na utapeli huo kwakuwa Rais Kikwete hajawapa kazi hiyo.
Baraza la mawaziri hadharani
      Leo huenda kiu ya Watanzania kujua nani ametoswa nani amekumbukwa kwenye Baraza la Mawaziri ikakatwa ambapo majina yao yataanikwa. Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari jana jijini Dar es Salaam na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Sefue, leo atakutana na waandishi wa habari Ikulu. Ingawa taarifa hiyo haikubainisha ni jambo gani litakalozungumzwa, suala la kutajwa kwa mawaziri wapya na mabadiliko ya baraza hilo ni jambo linalotarajiwa.
Source: Tanznia Daima (Jan. 2014). Mambo matatu yaitesa CCM. Retrieved from Tanzania Daima

No comments: