Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora

Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora
----------------------WE THANK AND APPRECIATE YOU FOR VISITING CHADEMA DIASPORA BLOG. AGAIN, THANK YOU!-----------------------

Sunday, December 29, 2013

Serikali yataja rasmi makundi ya kuunda Bunge Maalumu la Katiba

     Serikali imeyataka makundi mbalimbali ya watu yanayopenda majina yao kuteuliwa kuwa Wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, kufanya hivyo kabla ya Januari 2, 2014 saa tisa alasiri. Pia imeyaagiza makundi hayo kuzingatia sifa zilizotajwa kwenye Sheria ya Marekebisho ya Katiba wakati wa uteuzi wa majina ya watu watakaowapendekeza. Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Waziri wa Sheria na Katiba, Mathias Chikawe alisema kuwa makundi hayo yanatakiwa kuwasilisha kwa Rais orodha ya majina ya watu wasiopungua wanne na wasiozidi tisa. “Rais Jakaya Kikwete Desemba 13, 2013 alitoa tangazo kwa mujibu wa kifungu kidogo cha (2A) cha kifungu cha 22 cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, Sura ya 83 alialika kila kundi kutoka pande zote za Muungano kuwasilisha kwake majina kwa ajili ya kuzingatiwa kwenye uteuzi,” alisema Chikawe.
          Alibainisha kuwa kila kundi linatakiwa kuzingatia umri, jinsia, uzoefu, sifa na sehemu ya makazi ya mtu aliyependekezwa. Jumla ya idadi ya wajumbe kutoka Zanzibar hawatapungua moja ya tatu ya wajumbe wote. Chikawe alisema iwapo itabainika kuwa mtu aliyeteuliwa aliwahi kufungwa au kutokuwa na sifa, uteuzi wake utatenguliwa kwa kuwa atakuwa amepoteza sifa ya kuwa mbunge. “Hatuwezi kuwa na kundi la watu kutoka katika dini moja au kabila moja,” alisema. Akifafanua, alisema Bunge Maalumu la Katiba lina makundi matatu, ambapo wabunge wote wa Jamhuri ya Muungano, wajumbe wote wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar na watu 201 kutoka kwenye makundi mbalimbali watakuwa wajumbe.
           Akielezea mchanganuo wa watu kutoka makundi mbalimbali, alisema kuwa wajumbe 20 watatoka kwenye taasisi zisizokuwa za kiserikali, ambapo nusu yao lazima wawe wanawake na moja ya tatu kutoka Zanzibar. Pia watakuwepo wajumbe 20 kutoka taasisi zote za dini, wajumbe 42 kutoka vyama vyote vya siasa vyenye usajili wa kudumu. “Vipo vyama 21 kwa maana hiyo, kila chama kitaleta wajumbe wawili, mgawanyiko ni huohuo, kwa hiyo kwa vyama vya siasa hapa lazima mmoja atoke Zanzibar na mwingine Bara na lazima mmoja awe mwanamke na mwingine mwanaume,” alisema Chikawe. Wajumbe wengine na idadi yao kwenye mabano ni Taasisi za Elimu ya Juu (20), makundi ya watu wenye ulemavu (20), vyama vya wafanyakazi (19), vyama vinavyowawakilisha wafugaji (10), vyama vinavyowawakilisha wavuvi (10) na vyama vya wakulima 20.
          Chikawe alisema pia zimetengwa nafasi 20 kwa ajili ya wajumbe kutoka makundi mengine yoyote, ambayo yana malengo yanayofanana. Orodha ya majina hayo itawasilishwa kwa kupelekwa kwa Katibu Mkuu Kiongozi, Ikulu, Dar es Salaam au Katibu Mkuu Kiongozi, Ofisi ya Rais, Zanzibar. Pia Chikawe alitangaza kuwa Desemba 30, 2013, Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba atawasilisha taarifa kamili ya tume hiyo kwa Rais Jakaya Kikwete na Dk Mohammed Shein.
Source: Eliona G. (Dec. 2013).Serikali yataja rasmi makundi ya kuunda Bunge Maalumu la Katiba. Retrieved from Mwananchi

No comments: