Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora

Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora
----------------------WE THANK AND APPRECIATE YOU FOR VISITING CHADEMA DIASPORA BLOG. AGAIN, THANK YOU!-----------------------

Thursday, September 19, 2013

Hatuna ugomvi na CCM, JK-Wapinzani


  
      Viongozi wa vyama vikuu vya upinzani wamesema hawana ugomvi na CCM na kwamba wanawakaribisha kwenye meza ya majadiliano kwani Katiba sio jambo la kisiasa. Pia, viongozi hao wa vyama wamesema hawafikirii kuonana na Rais Jakaya Kikwete, kwani hawana ugomvi naye bali wana ugomvi na wabunge wanaofanya uamuzi bila kujitambua. Mbali na hayo wamesema wamesikitishwa na kauli ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu), Stephen Wassira aliyesema kwamba Ikulu imefungwa, ambapo viongozi hao walidai kuwa Ikulu ni mali ya kila Mtanzania na sio ya mtu binafsi. Kauli hizo zilitolewa Dar es Salaam jana na mmoja wa kiongozi wa vyama hivyo, James Mbatia ambaye ni Mwenyekiti wa NCCR- Mageuzi na Mbunge wa kuteuliwa baada ya kutolewa mapendekezo ya kuonana na Rais Kikwete.
           Mapendekezo hayo yalitolewa na Mjumbe wa Bodi ya Shirikisho la Vyama vya Watu wenye Ulemavu (Shivyawata), Amon Anastazia, wakati akitoa mapendekezo yake na maoni kuhusu mchakato wa Katiba unavyokwenda. Akizungumza wakati wa kufunga majadiliano hayo, mwenyekiti wa huyo alisema, kuungana kwao siyo kwamba wana ugomvi na CCM bali wameamua kutetea Watanzania kwa maslahi ya taifa. “Lengo letu ni kutaka kuona kwamba Katiba inapatika kwa maslahi ya Watanzania wote na kwamba sio kwa maslahi ya kisiasa au chama cha siasa,”alisema Mbatia na kuongeza; Kuna wabunge wanakwenda bungeni, lakini hawajui wanakwenda kufanya nini, mifano ya wazi mnaiona kuna wabunge kazi yao ni kuitikia tu ndiyooo…wakati hawajui nini kimejadiliwa au kimeongelewa kwa wakati huo na kwamba ugomvi wetu mkubwa ni watu kama hao. Tutazidi kupingana nao kwa nguvu zote,” alisema.
        Mjumbe wa bodi hiyo, Amon Anastazia ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Shivyawata alisema, “Tumefurahishwa na ujio wenu, lakini tunaomba mfanye juhudi za kukutana na Rais Kikwete ili muweze kuzungumza naye kwa pamoja kuhusu mchakato huu unavyo kwenda,”alisema na kungeza; “Kama mtafanya hivyo ikiwa pamoja na kuwasilisha mambo yote mnayo yajadili na kuyakusanya kutoa kwenye asasi za kiraia tuna imani yale ambayo mmeyakusudia Rais anaweza kuyafanyia kazi,” alisema Anastazia. Naye, Mwasisi wa Shivyawata ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha Watu Wenye Ulemavu wa Viungo (Chawata), Shida Salum alisema, “Watu wenye ulemavu ambao idadi yao ni milioni 7.9 walipeleka malalamiko yao Tume ya Katiba ili waeze kupewa nafasi ya uwakilishi, lakini maombi yao hayakufanyiwa kazi jambo ambalo limetusikitisha,”alisema na kuongeza:
      “Baadhi ya mambo yanayolalamikiwa ni pamoja na kukosekana kwa matumizi ya lugha za alama kitu kinachowanyima fursa walemavu kwenye mchakato huo,” Alilisisitiza wanasiasa hao kuwatete watu wenye ulemavu kwa nguvu kwani ndiyo njia pekee ya kuweza kuwasadia kupata kura kwenye chaguzi zijazo. Mbali ya hayo, shirikisho hilo limesema limesikitishwa kuona walemavu wamekosa fursa ya kutoa wawakilishi wengi kwenye mchakato huo, hivyo wanaamini watakosa haki zao za msingi kwenye Katiba ijayo kama itapita bila kushirikishwa. Katika mkutano huo wenyeviti waliofika kwenye ofisi za Shivyawata walikuwa ni pamoja na Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema ), Freeman Mbowe, Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba na Chama cha NCCR- Mageuzi, James Mbatia na baadhi ya viongozi wa vyama hivyo.
Source: Mhando A., & Shempemba R. (Sept. 2013). Hatuna ugomvi na CCM, JK-Wapinzani. Retrieved from Na Mwananchi

No comments: