Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora

Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora
----------------------WE THANK AND APPRECIATE YOU FOR VISITING CHADEMA DIASPORA BLOG. AGAIN, THANK YOU!-----------------------

Sunday, July 21, 2013

Dk. Slaa, Lowassa wawekewa mtego - Waliosafishiwa njia

*Rasimu kutumika kuwaondolea sifa ya kugombea urais

*Yumo pia Membe, Magufuli, Sitta, Zitto na Wassira


     MKAKATI wa kuwaengua vigogo wanaotajwa kung’ang’ania kugombea nafasi ya Urais katika Uchaguzi Mkuu mwaka 2015 sasa umebainika, MTANZANIA Jumapili linaripoti. Kwa mujibu wa uchunguzi wa kina uliofanywa na gazeti hili, mkakati huo ambao umelenga kuwang’oa viongozi hao, unadaiwa kutekelezwa na baadhi ya wanasiasa ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kupitia Rasimu ya Katiba Mpya, iliyotolewa hivi karibuni na Tume ya Mabadiliko ya Katiba. Imeelezwa kuwa kupitia Rasimu hiyo ya Katiba Mpya, kuna vipengele vilivyopenyezwa kwa nia ya kuwabana watu fulani fulani ndani na nje ya CCM ambao wanatajwa kuusaka ukuu wa dola mwaka 2015 na chama hicho hakitaki kuona wanakuwa kikwazo dhidi yake.
       Mtoa habari wetu ndani ya CCM alilidokeza gazeti hili kuwa vipengele hivyo ambavyo vimewekwa kama mtego, ni vile vinavyotaja sifa za mgombea Urais na mgombea Ubunge. Kwa mujibu wa taarifa zilizotufikia, kutokana na hilo, baadhi ya wanasiasa ndani ya CCM kwa makusudi wameamua kuufanya mjadala kuhusu serikali tatu kuwa mkali, ili kuzuia mjadala mpana katika masuala mengine. Kipengele ambacho kama kikiachwa bila kufanyiwa marekebisho kinaweza kuwabana wanasiasa wengi ndani na nje ya CCM wanaotajwa kuwania Urais 2015 ni pamoja na kile cha Sura ya Saba, ambacho kinazungumzia Serikali ya Jamhuri ya Muungano kuhusu Serikali, Rais na Makamu wa Rais, katika sehemu ya kwanza C kwenye kipengele cha 75 (E) kinachozungumzia sifa za Rais kimeeleza kuwa mtu atakuwa na sifa ya kuchaguliwa kushika nafasi ya madaraka ya Rais wa Jamhuri ya Muungano ikiwa: anazo sifa za kumwezesha kuwa Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano kwa mujibu wa Katiba hiyo.
       Wakati ikiwa hivyo katika sifa za kuwania nafasi ya Rais, kwenye Rasimu hiyohiyo kipengele cha sifa za kuwania nafasi ya Ubunge kilichopo katika sura ya tisa, sehemu ya pili (A) inayozungumzia kuhusu uchaguzi wa wabunge, katika kipengele cha (2a) kimeeleza kuwa mtu hatakuwa na sifa za kugombea/ kuchaguliwa kuwa Mbunge ikiwa mtu huyo aliwahi kuwa Mbunge kwa vipindi vitatu vya miaka mitano. Kutokana na hilo, ni wazi kuwa viongozi au vigogo waliowahi kuwa wabunge kwa vipindi zaidi ya vitatu vya miaka mitano hawatakuwa na sifa za kugombea Urais kwa sababu tayari kipengele cha sifa za kuwania Urais kimetaja kuzingatia sifa za mgombea ubunge. Kwa mujibu wa uchunguzi uliofanywa na gazeti hili, umebaini kuwa vigogo karibu wote ndani na nje ya CCM wanaotajwa kutaka kuwania nafasi ya Urais watakuwa wamepoteza sifa za kuwania nafasi hiyo endapo kipengele hicho kitaachwa bila kufanyiwa mabadiliko.

     Vigogo hao wanaotajwa kutoka CCM ni Waziri wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta, Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa, Waziri wa Ujenzi, Dk. John Magufuli, Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe.  Wengine ni Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk. Emmanuel Nchimbi na Naibu Waziri wa Sayansi na Teknolojia, Januari Makamba, wakati kutoka Chadema ni Mbunge wa Hai, Freeman Mbowe, Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk. Willbroad Slaa na Zitto Kabwe.

Watakaokuwa wametupwa nje

     Kulingana na sifa zinazotajwa kwenye kipengele hicho, viongozi wanaotajwa kutaka kuwania nafasi hiyo lakini watakuwa wamegonga mwamba ni pamoja na wafuatao;  Edward Lowasa ambaye aliwahi kuwa Waziri Mkuu kwa muda wa miaka miwili na hadi sasa ni Mbunge wa Monduli kupitia CCM, ameshika nafasi hiyo kwa vipindi vitano vya miaka 25 kuanzia mwaka 1990 hadi sasa, moja kwa moja atakuwa amepoteza sifa ya kuwania Urais, kwani tayari amezidi vipindi vitatu vya kuwa mbunge. Samuel Sitta, ambaye ni Mbunge wa Urambo Mashariki (CCM), ameshika nafasi hiyo kwa vipindi sita kwa muda wa miaka 30, kuanzia mwaka 1975 hadi 1995 na 2005 hadi sasa, naye pia atakuwa amepoteza sifa.

     Dk. John Magufuli, ambaye ni Mbunge wa Chato (CCM) kwa vipindi vinne vya miaka 20 kuanzia mwaka 1995 hadi 2015, naye atakuwa ameshapoteza sifa, kwani amezidi vipindi vitatu. Bernard Membe, ambaye pia ni Mbunge wa Mtama (CCM) naye atakuwa ametupwa nje, kwani hadi sasa ameshika nafasi hiyo ya Ubunge kwa vipindi vitatu vya miaka 15 kuanzia mwaka 2000 hadi 2015. Dk. Willborad Slaa, atakuwa ametupwa nje ya ulingo kwani amewahi kutumikia vipindi vitatu vya Ubunge kunzia 1995 hadi 2010 katika Jimbo la Karatu kwa kupitia Chadema. Zitto Kabwe ambaye ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini, atakuwa ametimiza sharti la kuwa mbunge kwa vipindi viwili, lakini atagonga mwamba katika sharti la umri, kwani atakuwa hajatimiza umri wa miaka 40 kama rasimu ilivyoendelea kupendekeza, badala yake atakuwa na umri wa miaka 39.

Waliosafishiwa njia

      Dk. Harrison Mwakyembe, ambaye ni Mbunge wa Kyela (CCM) ameshika nafasi hiyo vipindi viwili vya miaka 10 kuanzia mwaka 2005 hadi 2010. Dk. Emmanuel Nchimbi ambaye ni Mbunge wa Songea Mjini (CCM) ametumikia nafasi hiyo kwa kipindi kimoja cha ubunge wa jimbo kuanzia mwaka 2010 hadi sasa. Januari Makamba, ambaye ni Mbunge wa Bumbuli (CCM) amedumu kwa kipindi kimoja kuanzia mwaka 2010 hadi sasa hivyo atakuwa na sifa za kuwania urais. Freeman Mbowe, ambaye ni Mwenyekiti wa Taifa wa Chadema na Mbunge wa Hai, naye atakuwa na sifa ya kuwania nafasi hiyo, kwani atakuwa ametumikia nafasi hiyo kwa vipindi viwili kwa miaka 10 kuanzia 2000 hadi 2005 na 2010 hadi sasa. Suala la Urais limezua mjadala mkubwa ndani na nje ya CCM, baadhi wakikomoana kuhakikisha mwingine hapiti kwenye nafasi hiyo. CCM ndicho kinachoonekana kuathirika zaidi, kwani jambo hilo tayari limesababisha makundi yanayosigana.

Source:Mushi G. (July 2013). Dk. Slaa, Lowassa wawekewa mtego - Waliosafishiwa njia. Retrieved from Mtanzania

No comments: