Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora

Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora
----------------------WE THANK AND APPRECIATE YOU FOR VISITING CHADEMA DIASPORA BLOG. AGAIN, THANK YOU!-----------------------

Saturday, August 31, 2013

Wabunge waupinga Mwenge


  BAADHI ya wabunge wamekosoa mbio za Mwenge wa Uhuru, huku wengine wakitaka ufutwe kwa maelezo kuwa hauna tija kwa sasa. Wabunge hao wakiwamo wa upinzani na CCM, walisema Mwenge umekuwa kero na kwamba wakati mwingine ofisi za umma hufungwa kutokana na mbio zake na hivyo kusababisha wananchi kukosa huduma.

Hata hivyo Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, (Utawala Bora), George Mkuchika, alizomewa na kurushiwa maneno ya kejeli pale alipojaribu kujenga hoja ya kutetea mbio hizo za mwenge.

 

        Sakata hilo lilitokea jana bungeni, baada ya Mbunge wa Musoma Mjini Vicent Nyerere (Chadema), ambaye alitaka kujua faida na hasara zilizopatikana tangu Mwenge wa Uhuru ulipoanza kukimbizwa katika maeneo mbalimbali nchini.

Nyerere alisema wakati fulani viongozi wa Serikali walimtisha Naibu Meya wa Manispaa ya Musoma, Nyamero Bwire, kutokana na hatua yake ya kuzuia gari la wagonjwa la hospitali ya wilaya kutumika katika mbio hizo.

 Kutokana na hali hiyo, baadhi ya wabunge walimzomea Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Utawala Bora, Mkuchika, baada ya kuinuka na kutoa ufafanuzi wa swali hilo lililoulizwa na mbunge huyo.

Katika swali lake la msingi, mbunge huyo alisema kuwa tangu mwenge ulipohamishiwa katika mfumo wa Serikali, wananchi wamekuwa wakilazimishwa kuchangia fedha kwa nguvu pamoja na matumizi yasiyokuwa sahihi ya magari ya Serikali.

“Serikali haioni kwamba kuanzia sasa ianze kukimbiza mwenge katika maeneo yale tu ambayo wananchi wake wapo tayari kuchangia michango ya mwenge?” Alihoji Nyerere.

Mbunge huyo pia alitaka kujua kiasi cha bajeti ya mbio za mwenge kwa mwaka na iwapo matumizi ya fedha hizo hufanyiwa ukaguzi.


         Kwa upande wake Mbunge wa Nkasi Kaskazini, Ally Kesy (CCM), alisema mbio za mwenge hazina faida kwa Watanzania walio wengi kwani shughuli za kiuchumi zimekuwa zikiathiriwa. “Binafsi hiki kitu kinachoitwa mwenge sikitaki kabisa, kwani ni wazi tangu maandalizi yake hadi kufika kwake kumekuwa na mateso, kwani viongozi wanatakiwa kutoa huduma lakini wote huondoka ofisini. “Wanatumia siku tatu kwa ajili ya kukagua miradi inayoitwa ya mwenge, huku wananchi wakisota kuwasubiri na hata baada ya kufika na kukesha katika eneo husika. “Wakati mwingine hutumia siku mbili kupumzika badala ya kuwahudumia wananchi kwa kisingizio cha mwenge. Sasa tulipofika inatosha, ni vema mwenge usikimbizwe kwani umekuwa na matumizi mabaya,” alisema Kesy.

Mkuchika azomewa

       Katika majibu yake, Mkuchika alisema kuanzishwa kwa mwenge huo ulikuwa na lengo la kukimbizwa Tanganyika na hata kuwamulika maadui wa Tanzania. “Wale wanaodai kwamba mbio za mwenge hazina umuhimu si kweli. Malengo yake yalikuwa ni kukimbizwa Tanganyika na umekuwa ukitoa elimu kama vile elimu kuhusu dawa za kulevya, rushwa na kuzindua miradi ya maendeleo,” alisema Mkuchika. Majibu hayo yalimfanya akumbane na zomea zomea kutoka kwa wabunge wa kambi ya upinzani, huku zikisikika sauti za wabunge wakisema; “Mwenge unaeneza Ukimwi”, “unaeneza ufisadi na hatuutaki tena”.

          Baada ya jibu hilo baadhi ya wabunge walisimama na kutaka kuomba mwongozo wa Spika, huku Mbunge wa Wawi Hamad Rashid Mohamed (CUF), akitaka fedha za mwenge zikaguliwe. “Serikali huwa inatenga fedha kwa ajili ya mbio za mwenge, pia wananchi huchangishwa fedha kwa ajili ya mwenge huo huo, lakini fedha zake hazijulikani vizuri matumizi yake. “Tunataka CAG (Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali), afanye ukaguzi kwenye matumizi ya fedha za mwenge tangu ulipoanza kukimbizwa hadi sasa,” alisema. Naye, Mbunge wa Kasulu Mjini Moses Machali (NCCR-Mageuzi), alitaka Bunge liahirishwe ili kutoa fursa kwa wabunge kujadili hoja ya mwenge, ambao alisema hauna faida zaidi ya kuwasumbua wananchi.

      Mbunge wa Chakechake, Mussa Haji Kombo (CUF), aliomba mwongozo wa Spika akihoji kwanini mwenge unakimbizwa Zanzibar wakati uliasisiwa Tanzania bara. “Mheshimiwa Naibu Spika ninachotaka kusema hapa, Waziri Mkuchika alisema kuwa Mwenge ulianzishwa na ulikuwa ukimbizwe Tanganyika, je imekuwaje ukimbizwe Zanzibar,” alihoji. Awali akijibu swali la msingi la Nyerere, Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Amos Makala alisema alisema mbio za Mwenge wa Uhuru zilianzishwa kwa falsafa ya kuhamasisha ukombozi wa taifa na bara la Afrika, mwasisi wake akiwa ni Mwalimu Julius Nyerere.

     Alisema mwenge huo umeendelea kuwa tunu ya taifa na chombo pekee cha uzalendo kinachohamasisha na kuhimiza mshikamano, umoja wa kitaifa, uzalendo, uadilifu, kukuza moyo wa kujitolea na kuuenzi uhuru. Alisema Mwenge wa Uhuru utaendelea kukimbizwa na kwamba michango ya mbio hizo kwa wananchi ni ya hiari. Makala alisema ni kweli shughuli za mwenge hubadilisha ratiba katika wilaya husika, lakini faida za kukimbiza mwenge ni kubwa kuliko shughuli hizo, hivyo utaendelea kukimbizwa.

Source: Kimwanga B. (August 2013). Wabunge waupinga Mwenge. Dodoma. Retrieved from Mtanzania

No comments: