Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora

Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora
----------------------WE THANK AND APPRECIATE YOU FOR VISITING CHADEMA DIASPORA BLOG. AGAIN, THANK YOU!-----------------------

Thursday, August 29, 2013

Wabunge Tanzania watoka nje Bunge la Afrika Mashariki


     Wabunge wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA) kutoka Tanzania wametoka nje ya ukumbi wa Bunge ikiwa ni siku moja baada ya wenzao wa Rwanda na Uganda kufanya hivyo, wote wakipingana kuhusu utaratibu wa kufanya vikao vya bunge hilo. Juzi wakiunga mkono hoja iliyowasilishwa na Mbunge kutoka Kenya, Peter Mathuki, wabunge wote kutoka Rwanda na baadhi wa Uganda, walitoka nje ya ukumbi wa Bunge hilo wakishinikiza hoja iliyowasilishwa na mbunge huyo kuwa vikao vingine vifanyike nje ya makao makuu Arusha ikubaliwe. Wakati wabunge kutoka Tanzania wanapinga utaratibu unaopigiwa debe na wabunge kutoka nchi wanachama wakitaka kuwepo kwa mzunguko wa vikao vya bunge hilo, Watanzania wanataka utaratibu asilia wa EALA wa kuendesha vikao vyake makao makuu ya Jumuiya hiyo uendelee kuheshimiwa.

       Wabunge kutoka Tanzania wanapinga utaratibu wa kufanya vikao kwa kuzunguka kila nchi mwanachama kwa maelezo  kuwa kufanya hivyo ni kwenda kinyume na utaratibu wa kuanzisha Bunge hilo na ni gharama kwa uendeshaji. Katika kuonyesha hawaungi mkono utaratibu huo, wabunge kutoka Tanzania jana nao waliacha kuingia ukumbi wa Bunge ikiwa ni ishara ya kuonyesha hawakubaliani na ukiukwaji wa taratibu ya EALA. Mbunge kutoka Tanzania, Abdullah Hussein Mwinyi,  ndiye aliyesimama na kulieleza Bunge hilo kuwa kitendo kilichofanywa na wabunge wenzao kutoka Rwanda hakikuwa cha kistaarabu. Alisema kuwa, kitendo hicho ni dharau kwa kiti cha Spika na Bunge hilo kwani hoja iliyowasilishwa haikufuata utaratibu wa kibunge.

      Alisema anasikitishwa na kilichotokea juzi bungeni hapo kwa kuwa siyo utamaduni mzuri uliozoeleka kwa bunge hilo. “Huu ni udhalilishaji wa kiti cha Spika na kimechafua hata sifa ya Bunge lako, tunatakiwa kuweka utaratibu sawa ili kiti kiheshimiwe,” alisema. Hata hivyo, baada ya kueleza hoja hiyo wabunge wa Tanzania walitoka nje ya ukumbi huo na kusababisha kikao hicho kushindwa kuendelea, huku Mwinyi akizungumzia kitendo walichofanya wabunge kutoka Rwanda kuwa siyo cha kistaarabu. Mbunge mwingine kutoka Tanzania, Shy-Rose Bhanji, akizungumzia tukio hilo alisema kwa mujibu wa utaratibu wa kidemokrasia hatua ambayo wameichukua ni ya kujibu mapigo kama ishara ya kupinga kitendo kilichofanywa na wenzao. Kufuatia kutoka nje kwa wabunge hao, Spika wa EALA, Dk Margerth Zziwa, aliahirisha kikao hicho hadi leo huku akiendelea na vikao vya ndani. Kila nchi mwanachama ina wabunge tisa ambao wanafanya idadi ya wabunge 45.


Source: Ngunge J. (August 2013).Wabunge Tanzania watoka nje Bunge la Afrika Mashariki. Retrieved from Ippmedia/Nipashe

No comments: