Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora

Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora
----------------------WE THANK AND APPRECIATE YOU FOR VISITING CHADEMA DIASPORA BLOG. AGAIN, THANK YOU!-----------------------

Monday, August 5, 2013

Tendwa ang'oka


    JAJI wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dodoma, Francis Mutungi, ameteuliwa na Rais Jakaya Kikwete kuwa Msajili wa Vyama vya Siasa. Taarifa ya uteuzi huo iliyotolewa jana na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu na kutiwa saini na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue, ilisema kuwa uteuzi huo ulianza Agosti 2, mwaka huu. Jaji Mutungi anachukua nafasi iliyoachwa wazi na aliyekuwa Msajili wa Vyama vya Siasa, John Tendwa, ambaye amestaafu utumishi wa umma kwa mujibu wa sheria. Uteuzi huo unamfanya Jaji Mutungi kuwa msajili wa tatu tangu kurejeshwa tena mfumo wa vyama vingi nchini mwaka 1992. Aliyekuwa wa kwanza kukalia ofisi hiyo ya msajili ni Jaji mstaafu, George Liundi, kisha akafuatiwa na Tendwa, ambaye amerithiwa na Jaji Mutungi. Jaji huyo aliwahi kuwa Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania.

Wapinzani wasifu


    Kufuatia uteuzi huo mpya, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimesema kuwa Tendwa alipaswa kuwa ameondoka ofisini tangu mwaka 2008 alipofikisha umri wa kustaafu kwa mujibu wa sheria. Tarifa ya Kurugenzi ya Habari na Uenezi ya chama hicho imesema kuwa Tendwa alitumia muda huo wa miezi kadhaa alipoongezewa mkataba kuropoka na kuharibu demokrasia kwa manufaa ya Rais Kikwete na CCM. CHADEMA iliongeza kuwa kutokana na mwenendo wake mbovu, chama hicho kilitangaza kutokumpatia ushirikiano wowote kwa vile alikuwa adui wa demokrasia nchini. “Kwa muda wote huo, CHADEMA ilikuwa ikitoa ushirikiano kwa Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa. Badala ya kuifuta CHADEMA na kufanikisha dhamira ovu ya kuharibu amani ya nchi, ameondoka yeye,” ilisema taarifa ya CHADEMA.

     CHADEMA ilisema kuwa wanamkaribisha Jaji Mutungi kwenye kazi na majukumu yake mapya. Kwamba, wapenda demokrasia na maendeleo nchini wanamtarajia atatimiza wajibu wake kwa kuzingatia haki, sheria na utawala bora, asije akapita njia ya Tendwa. “Kupitia mchakato wa Katiba mpya unaojadiliwa sasa hivi, CHADEMA tunapendekeza Ofisi ya Msajili ipewe uhuru zaidi na uteuzi wake usiwe suala la rais kuamka tu na kuamua kuteua bila wahusika kuomba, kuchujwa na kuthibitishwa na mamlaka nyingine tofauti na iliyoteua,” walisema. Jaji Mutungi, anapaswa kuonesha kwa maneno na vitendo kwamba hatakuwa kama Tendwa, kwa kuanza kushughulikia matendo ya kiharamia yaliyofanywa na Green Guards wa CCM kwenye chaguzi za madiwani zilizomalizika hivi karibuni.

     Naibu Mkurugenzi wa Uenezi na Haki za Binadamu wa Chama cha Wananchi (CUF), Abdul Kambaya, alisema ni jambo zuri ingawa aliyemteua vilevile ni Mwenyekiti wa CCM, hatua ambayo inaleta hofu kidogo. “Tunadhani ni mtu mweledi, sisi hatupigi ramli kuhusu utendaji wake, mpaka tutakapomwona akianza kazi. Wakati wa Tendwa tumefanya kazi katika mazingira magumu, hasa sisi wapinzani, tunaomba huyu asifuate hayo. Tendwa aliiogopa sana CCM,” alisema. Naye Katibu Mkuu wa NCCR-Mageuzi, Sam Ruhuza, alisema wanamtakia kila jema Tendwa na kumkaribisha kwa furaha Jaji Mutungi, japokuwa wateule wote huwa wanafanya kazi ya kumpendeza aliyewateua.

Source: Tanzania Daima ( August 2013). Tendwa ang'oka. Retrieved from Tanzania Daima

No comments: