Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora

Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora
----------------------WE THANK AND APPRECIATE YOU FOR VISITING CHADEMA DIASPORA BLOG. AGAIN, THANK YOU!-----------------------

Monday, August 12, 2013

MOI: Jeraha la Ponda utata

AWEKWA CHINI YA ULINZI, HAKI ZA BINADAMU WALALAMA


   UTATA umezidi kuongezeka juu ya tukio la kujeruhiwa kwa Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu, Sheikh Ponda Issa Ponda, baada ya Kitengo cha Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Upasuaji wa Mishipa na Fahamu (MOI) kushindwa kubainisha kilichosababisha jeraha hilo. Hatua hiyo inazidi kuibua maswali kwa vile bado kuna mvutano kati ya ndugu na wafuasi wa Sheikh Ponda ambao wanadai kuwa alijeruhiwa kwa kupigwa risasi na askari, wakati Jeshi la Polisi linasisitiza kutohusika na tukio hilo. Wakati utata huo ukijitokeza, mashirika ya Utetezi wa Haki za Binadamu na Baraza la Waislamu nchini (BAKWATA), wametaka kuundwa kwa tume huru ya uchunguzi kuhusu tukio hilo huku mashirika hayo yakiahidi kuchangia rasilimali fedha. Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Ofisa Uhusiano wa MOI, Almas Jumaa, alisema baada ya Sheikh Ponda kupokewa juzi alionekana akiwa na jeraha chini ya bega la mkono wa kulia lililokuwa limeshonwa.

       Alisema baada ya uchunguzi wa madaktari walishauriana afanyiwe kipimo cha X-ray ambacho kilionesha kuwapo kwa mvunjiko bila mifupa kupishana. “Alipokuja alikuwa ameshafanyiwa tiba ya awali lakini kidonda kilikuwa katika hali mbaya, tukaona tumfanyie upasuaji mwingine kuzuia maambukizi,” alisema. Aliongeza kuwa licha ya kumfanyia upasuaji bado hali ya kubaini kitu kilichomsababishia jeraha hilo hakijajulikana na kwamba kwa sasa hali yake inaendelea vizuri. Akizungumzia tukio hilo, Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alhad Musa Salum, alisema ni vema serikali ikaunda tume huru ya uchunguzi. Alisema kuwa pamoja na BAKWATA kupingana na misimamo ya Sheikh Ponda, bado serikali ilikuwa na nafasi ya kumkamata na kisha kufuata mkondo wa sheria badala ya hatua ambayo imechukuliwa.

       Sheikh Alhad alisisitiza kuwa kabla ya tume hiyo kuanza kazi ni vema Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Morogoro, Faustine Shilogile, akajiuzulu ili kupisha uchunguzi huru wa tukio hilo. “Kujiuzulu kwa Kamanda Shilogile ni kwa sababu jeshi limehusishwa na yeye ndiye msimamizi wa askari katika Mkoa wa Morogoro, ni vema akae pembeni,” alisema. Alisema jamii inapaswa kutambua kuwa BAKWATA haina uadui na Sheikh Ponda, hivyo haiko tayari kuona anadhuriwa kwa namna yoyote.

Mashirika yanena

        Akisoma tamko hilo mbele ya waandishi wa habari kwa niaba ya mashirika hayo, Mratibu wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu, Onesmo Olengurumwa, alisema uundwaji wa tume hiyo utakuja na majibu yatakayoweza kuziridhisha pande zote badala ya iliyopo sasa ambayo imeundwa na polisi wakati wenyewe ni walalamikiwa. Olengurumwa alisema kutokana na uzoefu walionao na matukio yanayofanana na hayo, hawana imani kabisa na tume iliyoundwa kwa kuwa jeshi hilo linatuhumiwa kumjeruhi Sheikh Ponda wakati misingi ya haki za asili ikiwa haikubaliki mhusika kuwa hakimu kwenye shauri linalomhusu. Aidha, walitumia fursa hiyo kulaani utaratibu uliotumiwa na polisi katika kumkamata Sheikh Ponda mbele ya halaiki na wafuasi wake kwa madai kuwa lilikuwa ni tukio hatarishi kwa askari wenyewe pamoja na maisha ya raia.

      Katika wito wao, mashirika hayo yaliitaka Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora ambayo kikatiba ina jukumu la kufuatilia na kuchukua hatua kwa masuala kama haya ifanye hima kufuatilia na kuchukua hatua zote stahiki za kisheria. “Ikiwa tume itahitaji msaada wetu wa rasilimali watu na fedha tuko tayari ili iweze kufanya kazi hii kwa haraka kama inavyostahili, kwa kuwa tunaiamini, hasa pale ilipoweza kufanya uchunguzi wake katika mauaji ya mwandishi wa habari, Daudi Mwangosi na yale ya vurugu za Arusha, ila changamoto inakuja kwamba huwa inachukua hatua taratibu. “Pia tunaomba tume hii ifuatilie na matukio mengine mengi ya matumizi ya nguvu yanayofanywa na vyombo vya dola katika sehemu mbalimbali za nchi na kwa upande wa wananchi ni vema wawe watulivu na kuzingatia sheria za nchi katika kudai haki zao,” alisema.

        Naye Mkurugenzi wa Utetezi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Harold Sungusia, alivitaka vyombo vya dola vianze kujifunza kutenda haki kwa kuzingatia misingi ya haki za binadamu na utawala bora na kupendekeza kuwa mfumo wa Jeshi la Polisi uliopo sasa ni vema ukavunjwa kabla amani haijatoweka, kwa kuwa umekosa mwelekeo. Katika hili Sungusia alienda mbali zaidi na kutaka kuundwa kwa chombo kitakachoweza kulisimamia na kuliadhibu jeshi hilo pindi linapokwenda kinyume cha sheria, kwa kuwa sasa hivi linajifanyia mambo yake likijua hakuna wa kuliwajibisha. Akifafanua sheria ambayo inaeleza namna ya kumkamata mtuhumiwa, alisema kwenye sheria za kesi za jinai mtuhumiwa haruhusiwi kupigwa risasi, huku akionesha wasiwasi wake kuwa huenda kauli ya ‘piga tu’ ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, ndiyo ikawa imeanza kutekelezwa. Mkurugenzi wa Shirika la Sikika, Irenei Kiria, alisema kwa Morogoro hili tukio si la kwanza, jambo ambalo linaonesha wazi kwamba kuna uongozi mbovu wa jeshi katika mkoa huo.

Polisi wamkamta

        Kamishna wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, alisema kuwa wanamshikilia Sheikh Ponda kutokana na kutuhumiwa kukiuka masharti ya kifungo anachokitumikia. Hata hivyo, alifafanua kuwa ulinzi waliomuwekea kwa sasa ni kwa ajili ya kuzuia watu wasiweze kumdhuru. “Tumesikia matamko mbalimbali yanatolewa, sisi tupo imara kiulinzi na hatutamvumilia yeyote atakayekwenda kinyume cha sheria hapa Dar es Salaam, muhimu ni kwamba tunamlinda na kumshikilia Ponda kwa usalama wake,” alisema Kova.

Source: Tanzania Daima (August 2013).MOI: Jeraha la Ponda utata. Retrieved from Tanzania Daima

No comments: