Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora

Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora
----------------------WE THANK AND APPRECIATE YOU FOR VISITING CHADEMA DIASPORA BLOG. AGAIN, THANK YOU!-----------------------

Sunday, August 11, 2013

CCM na hulka ya kupinga mambo ya maana



MAKALA: KITILIA MKUMBO

MJADALA kuhusu Rasimu ya Katiba Mpya umeanika sura halisi ya Chama cha Mapinduzi (CCM). Kwamba wamepinga mambo yote ya maana katika rasimu hiyo si jambo la ajabu na inatukumbusha kwa mara nyingine kwamba chama hiki kitasimama kinyume na jambo lolote linalotishia uhai wake madarakani, hata kama jambo hilo ni la manufaa kiasi gani kwa nchi.
    
     Ukiacha suala la serikali tatu, katika rasimu inayoendelea kujadiliwa na mabaraza ya katiba, CCM wamepinga pia uwepo wa haki za binadamu ndani ya Katiba na kuingizwa kwa maadili katika Katiba mpya. Kupinga kuingizwa kwa haki za binadamu ndani ya Katiba ni kiashiria muhimu kwamba Chama cha Mapinduzi na serikali yake ni wavunjifu wa haki hizi na wana mpango wa kuendelea kuzivunja lakini sasa wanaogopa zikiingia kwenye Katiba zitawatia kitanzini.
     
   Kupinga kwao kuingizwa kwa maadili ndani ya Katiba ni kiashiria kingine kwamba chama hiki na serikali yake hawataki vitendo vya ufisadi vikome hapa nchini. Ikumbukwe kwamba suala la maadili liliingizwa katika rasimu kutokana na wananchi wengi waliotoa maoni kuhusu Katiba mpya kupigia kelele suala la ufisadi unaofanywa na viongozi. Ni kwa sababu hii tume wakatafsiri kwa usahihi kabisa kwamba ni muhimu maadili iwe sehemu ya Katiba ili vitendo vyovyote vya ufisadi vitakavyofanywa na kiongozi ijulikane kwamba kiongozi huyo amevunja Katiba na hivyo anastahili kupoteza madaraka yake wakati hatua za kisheria zikiendelea kuchukuliwa dhidi yake. Upinzani wa CCM dhidi ya maadili haushangazi kwa sababu wangeunga mkono vipi maadili iwe sehemu ya Katiba wakati uwepo wao madarakani unatokana na kukiuka maadili?


       Pamoja na kupinga mambo mengine katika Katiba mpya, CCM wanapaza zaidi sauti zao katika kupinga rasimu juu ya serikali tatu. Na katika kuimarisha upinzani wao dhidi ya serikali tatu wanatumia zaidi hoja ya gharama. Kwamba kuendesha serikali tatu ni gharama kubwa kuliko kuendesha serikali mbili na hivyo uwepo wa serikali tatu ni kuibebesha nchi na walipa kodi gharama za ziada zisizo za msingi.
      
      CCM wametumia mwanya wa Watanzania wengi kutokuhoji mambo kuipenyeza hoja hii dhaifu kwa kasi kubwa, na wananchi wanaelekea kukubaliana nao bila kuuliza maswali ya msingi. Katika kujenga hoja yao pinzani dhidi ya serikali tatu CCM hawatuambii ni kiasi gani cha gharama kinatumika sasa hivi katika kuendesha serikali mbili, na kiasi gani kitatumika katika kuendesha serikali tatu ili tupime tofauti ya hizo gaharama.

        Hawakokotoi hesabu hizi kwa sababu wanajua kwamba ukweli utajulikana na hoja yao itakosa nguvu. Kwa hivyo, hakuna ushahidi wowote wa maana unaoonyesha kwamba gharama za kuendesha serikali tatu itakuwa kubwa kuliko ile ya kuendesha serikali mbili. Kama CCM wangekuwa na uchungu kweli juu ya gharama za kuendesha serikali tatu wangepigania uwepo wa serikali moja ya Muungano ambayo kwa vyovyote gharama zake zingekuwa ndogo zaidi kuliko kuendesha muundo wa serikali mbili au tatu. Kwa hivyo, kama alivyopata kueleza mwanasiasa machachari na msomi wa sheria na haki za binadamu Tundu Lissu, hoja ya gharama za kuendesha serikali ina lengo la kuwatoa wananchi kwenye mjadala wa msingi juu ya umuhimu wa Katiba mpya na matatizo ya muundo wa Muungano ulivyo sasa.

      Ukweli ni kwamba hata ukifanya hesabu za haraka haraka utakuta kwamba gharama za serikali tatu zitakuwa ndogo zaidi kuliko serikali mbili. Nitatoa mfano katika eneo moja la Bunge. Kwa mujibu wa Rasimu ya Katiba Mpya, kutakuwa na wabunge wa Muungano 75. Bunge la Zanzibar litakuwa na wabunge 50 watakaotokana na majimbo ya sasa, na Bunge la Tanganyika litakuwa na wabunge 189 wa majimbo ya uchaguzi ya sasa. Kwa hiyo ukijumlisha hapa utaona kwamba mabunge yote matatu ya Muungano, Tanganyika na Zanzibar yatakuwa na idadi ya jumla ya wabunge 314.

       Ukilinganisha na Muungano uliopo sasa hivi ambapo tuna idadi ya wabunge 239 wa majimbo ya Muungano, wabunge wa viti maalumu 102, wabunge 10 wa kuteuliwa na Rais, wabunge watano wanaowakilisha Baraza la Wawakilishi, pamoja na Mwanasheria Mkuu tunapata jumla ya wabunge  357 wa Bunge la Muungano pekee.

        Tukijumlisha na wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wapatao 81 waliopo sasa hivi tunapata jumla ya wabunge 438! Kwa hiyo utaona hapa kwamba gharama za kuendesha mabunge katika muundo wa Muungano wa serikali tatu itakuwa ndogo kwa upungufu wa wabunge 124 ukilinganisha na mfumo wa sasa. Hali itakuwa ni hii hii tukifanya hesabu za kuhudumia taasisi mbalimbali za serikali katika muundo wa serikali tatu dhidi ya mbili.

      Ndio maana ninasema CCM wanazungumza juu juu na hawataki kwenda ndani kwa sababu wanajua wataumbuka na hoja yao itakufa. Bahati mbaya makada wa CCM wamezoeshwa kubebeshwa hoja kama kasuku na hawajafundishwa kutafakari. Wamejazana kwenye mabaraza ya katiba na wanaimba kama kasuku kwamba muundo wa serikali tatu ni gharama bila ushahidi wowote wa kimantiki na kihesabu. 

      Inabidi tukumbushane vilevile kwamba hoja ya serikali tatu haijaanza leo na mara zote imeibuliwa ndani ya CCM yenyewe. Hoja hii iliibuliwa  rasmi mara ya kwanza miaka ya 1990 wakati wa mjadala wa uwepo au kutokuwepo vyama vingi uliokuwa ukiendeshwa na Tume ya Jaji Mkuu Marehemu Francis Nyalali. Jaji Kisanga naye aliibua hoja hii mwaka 1998 wakati wa mjadala wa mabadiliko ya katiba. Majaji hawa kama, ilivyo kwa Jaji Warioba, waliteuliwa na marais wa CCM na baadhi yao kama Warioba wanajulikana kwa ukada wa CCM kuliko vijana wanaoibukia leo.

          Kabla ya hapo mwaka 1993 wabunge machachari 55 wa CCM walipeleka hoja bungeni ya kutaka kuundwa kwa serikali ya Tanganyika ndani ya Muungano, na hoja ilikuwa ipite kama Mwalimu Nyerere hakuingilia kati. Katika Gazeti la Uhuru la Jumatatu ya Agosti 5, 2013 amekaririwa Nape akijinasibu kwamba wanaotaka serikali tatu hawana akili timamu. Nami namuuliza Nape kati yake na hao majaji niliowataja hapo juu ni nani asiye na akili timamu?

          Kama nilivyosema mwanzoni mwa makala hii, CCM hawana hulka ya kuunga mkono mambo mema kwa nchi hii. Tukumbuke kwamba ni CCM hawa hawa waliopinga uwepo wa vyama vingi. Wakawalisha maneno makada wao waliotapakaa nchi nzima wakatae mfumo wa vyama vingi na ikawa hivyo. Hata hivyo, busara za kawaida za Mwalimu Nyerere ziliokoa jahazi na tukaingia kwenye mfumo wa vyama vingi huku CCM wakiwa hawajaridhia wala kuridhika.

          Ndio maana hadi leo CCM wanaamini kwamba wenyewe ndio chama pekee kinachostahili kuongoza nchi na vingine vipo tu kwa ajili ya kuonyesha kwamba tupo katika mfumo wa vyama vingi ili tupate misaada ya wazungu. CCM hawahawa pia walipinga kuwepo kwa katiba mpya na wakaapa kwamba hili ni jambo lisilowezekana nchini Tanzania. Wakamtumia mwanasheria mkuu na waziri wa sheria wa wakati huo kupiga kelele barabarani wakijanadi waziwazi kwamba suala la katiba mpya tusahau na halipo. Kilichookoa jahazi ni kujitoa ‘muhanga’ kwa Rais Kikwete ambaye aliamua binafsi kwamba kuna haja ya mchakato wa Katiba mpya. Naamini hii ngwe iliyobaki, ambayo ni ngumu zaidi, ni Rais Kikwete pekee atakayeokoa jahazi kwa kuwakemea makada wenzake waweke mbele maslahi mapana ya nchi hii dhidi ya maslahi mafupi na hafifu ya chama chao.

         Bila Rais Kikwete kujitoa ‘muhanga’ kama alivyofanya katika kuanzisha mchakato wa Katiba mpya tutakwama na nchi itaingia katika mgogoro usio wa lazima wa kisiasa. Yote hii ni kwa sababu makada wa CCM wametapakaa katika kila chombo kitakachoshughulikia Katiba mpya, kuanzia kwenye mabaraza hadi kwenye Bunge la Katiba.  Bahati mbaya makada wengi wa CCM hawajitegemei kimawazo na wanasubiri kuelekezwa cha kusema na chama chao na hapa ndipo umuhimu wa Rais Kikwete unapoingia. Hivyo, tunamsihi Rais Kikwete asikubali CCM wamtibulie alama ya utawala wake ambayo ni katiba mpya.  Ni muhimu ahakikishe kwamba jahazi alilolianzisha linafika mwisho salama na hii ndio itakuwa alama kubwa zaidi ya utawala wake.

No comments: