Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora

Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora
----------------------WE THANK AND APPRECIATE YOU FOR VISITING CHADEMA DIASPORA BLOG. AGAIN, THANK YOU!-----------------------

Friday, August 30, 2013

JK: CCM ijiandae kisaikolojia


    LICHA ya Chama cha Mapinduzi (CCM), kutangaza msimamo wa kukataa serikali tatu, Mwenyekiti wa chama hicho, Rais Jakaya Kikwete, amewataka wake wajiandae kisaikolojia kwa mabadiliko yoyote yatakayotokea kinyume na matakwa yao. Kwa mujibu wa chanzo kimoja kutoka ndani ya kikao cha Baraza la Kikatiba la Halimashauri Kuu ya CCM ambalo linapitia vifungu vya rasimu ya Katiba Mpya, Rais Kikwete aliwataka makada wenzake kujiandaa kwa lolote kama ilivyotokea mwaka 1992. Rais Kikwete alisema mwaka 1992 idadi kubwa ya wanachama wa CCM walikataa mfumo wa vyama vingi lakini mfumo huo ulipita.
Kiongozi huyo alisema katika kikao hicho cha mwaka 1992 ilikubalika kuwa ‘wengi wapewe wachache wasikilizwe’.

       Katika kikao cha jana Kikwete aliwataka wana CCM wajiandae kisaikolojia kwa jambo lolote litakaloamriwa na wananchi watakaopiga kura juu ya rasimu ya Katiba mpya. Kwa mujibu wa chanzo cha Tanzania Daima, Katibu wa Halmashauri Kuu ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa, Dk. Asha Rose Migiro, aliwasilisha na kuchambua upungufu uliopo kwenye rasimu ya Katiba Mpya iliyotolewa hivi karibuni na Tume ya Mabadiliko ya Katiba. Kutokana na upungufu huo hasa katika mfumo wa serikali idadi kubwa ya makada wa chama hicho ilikubaliana kuendelea na msimamo wao wa serikali mbili. Mara baada ya Migiro kumaliza, walisimama wajumbe kadhaa na Kikwete kumpa nafasi mmoja wao ambaye alitaka wasiendelee na suala la Katiba mpya liahirishwe mpaka baada ya mwaka 2015.

        Inaelezwa kuwa mjumbe huyo kutoka Zanzibar, alijenga hoja kuwa suala la Katiba mpya halikuwa kwenye ilani ya uchaguzi wa chama hicho ya mwaka 2010. Mjumbe huyo alisema ilani ya chama hicho ilitoa ahadi za ujenzi wa madaraja, barabara, ununuaji wa meli na nyinginezo nyingi ambazo mpaka sasa bado. Alisema ni busara CCM ikaachana na hoja hiyo mpaka baada ya uchaguzi wa mwaka 2015. Hata hivyo baada ya mjumbe huyo kutoa hoja hiyo, Kikwete aliwataka wajumbe wajadili mantiki ya rasimu ya Katiba mpya badala ya kufoka au kubishana. Rais Kikwete alisema mazingira ndiyo huamua jambo fulani hivyo hakuna sababu hoja hiyo ya Katiba kutojadiliwa hivi sasa.

       Inaelezwa kuwa Rais alisema licha ya asilimia 80 ya Watanzania kutoukubali mfumo wa vyama vingi mwaka 1992 hoja hiyo ilipita kutokana na mazingira. Alisema licha ya hofu ya Watanzania juu ya mfumo wa vyama vingi bado mfumo huo umendelea kuwepo mpaka hivi sasa na umeonyesha maendeleo. Baada ya kauli hiyo wajumbe walianza kupitia kifungu kwa kifungu Rasimu ya Katiba mpya ambapo wengi walipinga muundo wa serikali tatu uliopendekezwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.

Msimamo wa CCM

      Chama hicho tawala tangu kutoka kwa Rasimu ya Katiba kimekuwa kikisisitiza msimamo wa kutambua serikali mbili na si tatu kama ilivyotolewa na Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji mstaafu Joseph Warioba. Kamati Kuu (CC) iliyoketi Juni mwaka huu iliamua kuipeleka rasimu hiyo kwa wananchi wake kuanzia ngazi ya matawi na kutaka yaundwe mabaraza ya Katiba ya chama hicho. Hata hivyo CCM ilishaweka wazi msimamo wake kuwa haitokubali muundo wa serikali tatu. Akizungumza na Tanzania Daima, kabla ya kuingia katika kikao jana jioni, Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alisema suala la Katiba limewachukua nafasi kubwa.

     Alisema suala hilo limechukua muda mwingi kutokana na kupitia kifungu kwa kifungu na mpaka jana saa 10, walikuwa wamepitia vifungu 140. “Tumeshindwa kuanza kikao cha Halmashauri Kuu (NEC) kama tulivyotarajia kutokana na majadiliano hayo lakini nina imani tutamaliza vizuri.” Nape alisema suala la kuingizwa kwa uraia wa nchi mbili katika Katiba Mpya nalo liliteka zaidi mjadala.

Source: Mohamed S. ( August 2013).JK: CCM ijiandae kisaikolojia. Retrieved from Tanzania Daima

No comments: