Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora

Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora
----------------------WE THANK AND APPRECIATE YOU FOR VISITING CHADEMA DIASPORA BLOG. AGAIN, THANK YOU!-----------------------

Thursday, August 8, 2013

CHAMA CHA DEMOKRASIA NA MAENDELEO (CHADEMA)


MSIMAMO KUHUSU RASIMU YA KATIBA MPYA YA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
MAMBO MUHIMU YA KUZINGATIA

UTANGULIZI

Ndugu Msomaji wa “Msimamo wa CHADEMA kuhusu Rasimu ya Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania: Mambo Muhimu ya Kuzingatiwa”,

Katiba ni uhai wa Taifa lolote. Katiba ndiyo inayotuunganisha Watanzania, bila kujali itikadi zetu, dini zetu, jinsia zetu, rika letu, makabila yetu, hali zetu na tofauti zetu zozote. Katiba tunaweza kuiita Sheria Mama katika nchi. Hivyo hii ni fursa pekee kwako Mtanzania kushiriki katika zoezi la kuandika Katiba mpya ya Tanzania. Katiba zote zilizopita, pamoja na kuandikwa maneno ya kuvutia:-

" Kwa kuwa, Sisi Wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tumeamua rasmi na kwa dhati kujenga katika nchi yetu jamii inayozingatia misingi ya uhuru, haki, udugu na amani"'

"Na Kwa kuwa misingi hiyo yaweza tu kutekelezwa katika jamii yenye demokrasia ambayo Serikali yake husimamiwa na Bunge lenye wajumbe waliochaguliwa na linalowakilisha wananchi, na pia yenye mahakama huru zinazotekeleza wajibu wa kutoa haki bila woga wala upendeleo wowote, na hivyo kuhakikisha kwamba haki zote za binadamu zinadumishwa na kulindwa na wajibu wa kila mtu unatekelezwa kwa uaminifu":-

"Kwa hiyo basi, Katiba Hii ( ya mwaka 1977) imetungwa na Bunge Maalum la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa NIABA ya WANANCHI....".

Pamoja na maneno hayo yenye kuleta matumaini katika Katiba ya sasa, yaani ya Mwaka 1977, watanzania hawajawahi kushirikishwa kutunga Katiba ya Taifa lao. Katiba hiyo ilitungwa na Chama Tawala na Serikali "kwa niaba yao", Bunge lilitumika kama muhuri kwa kuhalalisha maamuzi ‘yao’.

Safari hii , Katiba Mpya inayoandikwa sasa, kuanzia hatua ya kukusanya maoni ya wananchi, kujadili na kupitisha rasimu ya katiba katika Bunge la Katiba na kuhalalisha katiba hiyo kupitia kura ya maoni; utaratibu wa kisheria wa ushiriki na uwakilishi wa wananchi umewekwa ingawaje upo upungufu ambao tutaendelea kuwaunganisha watanzania urekebishwe.

Ili kupata Katiba bora, inayobeba matarajio yetu Watanzania, ni muhimu wananchi kuwa macho na mtu yeyote anayetaka kuhujumu Katiba mpya kwa malengo yake binafsi au ya Chama chake. Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kinasisitiza, wananchi mkiona ubinafsi wetu katika Mapendekezo haya, yakataeni. Hivyo hivyo kwa Chama kingine chochote, ikiwemo Chama cha Mapinduzi (CCM). Yatazamwe maslahi ya Taifa, na mapendekezo ya chama kisichowakilisha maslahi ya wananchi na ya Taifa katika ujumla wake yakataliwe bila kumumunya maneno.

Ni kwa msingi huo, Kamati Kuu ya CHADEMA, iliketi tarehe 6 na 7 July, 2013 katika Hoteli ya Blue Pearl Jijini Dar-Es--Salaam, na kupitia kwa kina " Rasimu ya KATIBA ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, 2013". Aidha, kikao hicho cha kamati kuu kilichambua kwa kina unaoitwa " Ufafanuzi kuhusu Rasimu ya Kwanza ya Katiba kwa wanachama na viongozi wa CCM". Baada ya kutafakari kuhusu nyaraka hizo, Kamati Kuu imefanya maamuzi ya kutoa msimamo wa CHADEMA kuhusu rasimu ya katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wenye kueleza mambo muhimu ya kuzingatiwa.

Pia, kamati kuu iliazima kwamba msimamo huu ufikishwe kwa njia mbalimbali kwa viongozi na wanachama wa CHADEMA kote nchini, wapenzi wa chama na watanzania wote kwa ujumla wenye mapenzi mema na Taifa letu. Kamati Kuu imebaini mambo kadhaa yanayoashiria kuwa wananchi wasipokuwa makini na kusimamia maoni yao itatengezwa Katiba ya Serikali na CCM badala ya katiba ya Watanzania.

Tunao ushahidi kamili kuwa: CCM wamedhamiria mambo yote wanayotaka wao hata Kama siyo matakwa ya Watanzania yaingizwe ndani ya Katiba Mpya kwa njia yeyote ile. Tunataarifa za kina kutoka maeneo mbalimbali juu ya wanayoyafanya kutimiza azma yao dhidi ya makundi mengine katika jamii na wananchi kwa ujumla.

Kitendo cha CCM kuwapa msimamo katika vikao vya ndani wajumbe wa Mabaraza ya Wilaya waliochaguliwa na wananchi kupitia mikutano ya vijiji ni ishara ya wazi wa yote tuliyotahadhirisha juu ya uchujaji wa wajumbe kwenye kazi ya kata zenye kuhodhiwa na CCM. Sasa hali hiyo inatumiwa kuathiri maoni katika hatua ya mabaraza ya katiba yanayosimamiwa na tume ya mabadiliko ya katiba.

CCM inafanya matendo hayo kwa kuwa haikuwahi kuwa na dhamira ya kweli ya kuandika katiba mpya. Katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM, ajenda ya Katiba Mpya haikuwepo kabisa. Ajenda hiyo ilikuwa ndani ya Ilani ya CHADEMA na ilikuwa kati ya masuala muhimu katika mikutano ya kampeni ya wagombea wa CHADEMA wa udiwani, ubunge na urais.

Viongozi wakuu wa chama hicho wakati wote walikuwa wakiibeza ilani ya CHADEMA kuhusu kuanzisha mchakato wa katiba mpya ndani ya siku 100 iwapo CHADEMA ingeongoza Serikali. Shinikizo la wananchi ambalo liliongezewa msukumo na uamuzi wa wabunge wa CHADEMA kususia Hotuba ya Rais ya Ufunguzi wa Bunge wakidai mabadiliko kuliwafanya walegeze msimamo.

Hatua ilitanguliwa na kauli za viongozi waandamizi wa Serikali ya kwamba “hakuna haja ya kuwa na katiba mpya”. Katika hali kama hiyo, tusipochukua hatua watahujumu mchakato wa katiba na hivyo Tanzania kupata katiba mpya isiyokuwa bora.

Hali hii inathibitishwa na maudhui ya waraka huo ulioitwa "ufafanuzi..." uliotolewa na CCM ambao kimsingi unapinga mambo mengi muhimu katika rasimu ya katiba iliyotolewa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba inayoongozwa na Jaji (Mstaafu) Joseph Warioba.

Kati ya mambo wanayoyapinga ni pamoja na uwepo wa Serikali Tatu; yaani Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Serikali ya Zanzibar na Serikali ya Tanzania Bara. Msimamo wa CHADEMA umeeleza mambo muhimu ya kuzingatiwa kuhusu muundo wa Muungano wa Serikali tatu kwa mustakabali mwema wa taifa letu.


CCM hawataki hata Tunu ya " UWAZI" uwepo kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano katika hali ile ile ya kuruhusu mianya ya kulea “UFISADI”. CHADEMA kupitia msimamo huu imeunga uwazi kuingia katika katiba na kutoa maoni ya tunu nyingine muhimu za kuongezwa katika rasimu ya Katiba sanjari na kusimamia kwamba maadili na miiko ya uongozi iwe sehemu ya mambo ya Muungano.

CCM inakataa haki za msingi za watanzania zinazohusu masuala ya ardhi, maliasili na rasilimali ziingie katika katiba ya Jamhuri ya Muungano. CHADEMA kupitia msimamo huu imetoa maoni ya namna vifungu vya haki za binadamu vilivyomo vinavyopaswa kuboreshwa na kusimamia kwamba haki muhimu ikiwemo juu ya rasilimali za nchi na maisha ya wananchi ziwe sehemu ya mambo ya Muungano.

Mambo hayo na mengine yapo katika kijitabu hiki chenye sehemu saba za “Msimamo wa CHADEMA kuhusu rasimu ya katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania: Mambo Muhimu ya Kuzingatiwa”. Soma, chambua, tafakari na chukua hatua. Ukishasoma sambaza msimamo huu kwa wengine ili watoe maoni tupate katiba bora. Natanguliza shukrani za dhati.
Mabadiliko ya Kweli, Uhuru wa Kweli.

Dr Willibrod Peter Slaa
KATIBU MKUU
CHADEMA Julai 2013 

No comments: