Chama cha Demokrasia na Maendeleo
(Chadema) kimesema kitayaweka hadharani maoni ya wapenzi, wafuasi na wanachama
wake yaliyokusanywa nchini kote, kwenye mabaraza ya katiba, keshokutwa. Maoni hayo yalikusanywa na Chadema
katika mikutano ya ndani na hadhara, kwa njia ya mtandao, simu (sms), barua
pepe na maoni ya matawi ya chama hicho nje ya nchi. Ofisa Mwandamizi wa Habari wa
Chadema, Tumaini Makene, alisema kupitia taarifa yake kwa vyombo vya habari
jana kuwa maoni hayo yatawekwa hadharani baada ya kamati ndogo ya katiba ya
Kamati Kuu (CC) ya chama hicho kumaliza kuandaa ripoti yake.
Alisema ripoti hiyo itaandaliwa na
CC baada ya kuyaweka maoni hayo pamoja, kabla ya kuwasilishwa kwa Tume ya
Mabadiliko ya Katiba. Tangu Agosti 12, mwaka huu, Chadema
imekuwa kwenye operesheni maalum ya kukusanya maoni hayo, iliyokuwa ikifanywa
na timu mbili, zikiongozwa na Mwenyekiti, Freeman Mbowe na Katibu Mkuu, Dk.
Willibrod Slaa, kwa kutumia usafiri wa helkopta. Kwa mujibu wa Makene, operesheni
hiyo ilifanyika hadi juzi na ilifanikiwa kufika mikoa yote ya Tanzania Bara,
isipokuwa mikoa ya Lindi na Mtwara.
Alisema baada ya kumaliza mzunguko
wa kwanza kwenye wilaya za Tanzania Bara, viongozi wakuu wa Chadema watakwenda
Zanzibar kuhitimisha mchakato wa ukusanyaji maoni kuhusu Rasimu ya Katiba. Pia alisema chama kinaendelea
kupokea maoni kutoka mikoa ya Lindi na Mtwara, ambao wanaendelea kukutana
katika mabaraza ya ndani.
No comments:
Post a Comment