RAIA wa China, Xu Wenze (29)amefikishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi ya Wilaya ya Mpanda kwa tuhuma za kukamatwa na meno matatu ya fisi. Mwendesha Mashitaka wa Hifadhi ya Taifa ya Katavi, Pele Malima alidai mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi, Chiganga Tengwa kuwa mhuhumiwa huyo alitenda kosa hilo Januari 3 mwaka huu.
Alidai Mchina huyo anayeshiriki ujenzi wa barabara kutoka Mpanda hadi Sitalike alikamatwa na meno hayo matatu akiwa kwenye uwanja wa ndege wa Mpanda. Malima alidai mtuhumiwa alikamatwa na meno hayo muda mfupi kabla ya kupanda ndege iliyokuwa ikienda Mwanza. Mtuhumiwa huyo alifikishwa mahakamani hapo kwa mara ya kwanza wiki iliyopita akituhumiwa kukamatwa na meno matatu ya simba yenye thamani ya Sh 73,000,000.
Hata hivyo, Mwanasheria wa Serikali wa Mikoa ya Rukwa na Katavi alimbadilishia mashitaka kutoka ya kuhujumu uchumi na kuwa kesi ya kupatikana na nyara za Serikali. Mhuhumiwa alikana shitaka na yuko nje kwa dhamana wa Sh milioni tano na hati yake ya kusafilia imezuiwa hadi kesi yake itakapokwisha. Hakimu Chiganga aliahirisha kesi hiyo hadi Aprili 29 mwaka huu itakapotajwa tena.
Source: Mguluchuma W. (March 2013) Raia wa China kortini kwa kukutwa na meno ya fisi. Retrieved from Mtanzania
No comments:
Post a Comment