Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora

Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora
----------------------WE THANK AND APPRECIATE YOU FOR VISITING CHADEMA DIASPORA BLOG. AGAIN, THANK YOU!-----------------------

Tuesday, January 29, 2013


MAELEZO KWA WANAHABARI KUHUSU MAAMUZI YA MKUTANO MAALUM WA BARAZA KUU LA CHAMA CHA DEMOKRASIA NA MAENDELEO  (CHADEMA) ULIOFANYIKA TAREHE 28 JANUARI 2013 KATIKA UKUMBI WA DIAMOND JUBILEE JIJINI DAR ES SALAAM

Baraza Kuu la Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) limefanya mkutano wake maalum tarehe 28 Januari 2013 katika ukumbi wa Diamond Jubilee Jijini Dar es salaam ambao ulikuwa na ajenda zifuatazo: Maoni na Mapendekezo kuhusu Maudhui na mchakato wa katiba mpya; Mapendekezo ya Haja ya kufanya marekebisho katika kanuni za chama na kutunga muongozo; Mpango Kazi, Mkakati na mwendelezo wa Operesheni ya M4C na Bajeti ya chama kwa mwaka 2013 na mengineyo.

Baraza kuu limefanya maamuzi mbalimbali; katika hatua ya sasa tunatoa taarifa kwa umma kuhusu maazimio yafuatayo:

Maoni na Mapendekezo kuhusu Maudhui na mchakato wa katiba mpya

Baraza Kuu limepokea na kuridhia taarifa ya kamati kuu kuhusu maoni na mapendekezo ya chama kuhusu maudhui na mchakato wa katiba mpya. Baraza Kuu limezingatia kuwa katika mpya bora ni nyezo muhimu ya ufumbuzi wa matatizo ya kiongozi na migogoro inayolikabili taifa ikiwemo kuhusu rasilimali za nchi. Taarifa ya maamuzi ya Baraza Kuu kuu juu ya hatua zitazochukuliwa kuhusu maudhui na mchakato wa katiba mpya itatolewa kwa umma.

Kwa sasa umma ufahamu kwamba kati ya maamuzi hayo ni pamoja na kuridhia kwamba katika ya masuala ambayo CHADEMA itahamasisha umma kuikataa katiba mpya iwapo hayataingizwa ni pamoja na Katiba kutambua kwamba Wananchi ndio wamiliki wa rasilimali asilia za maeneo wanakoishi Kama vile ardhi, madini, mafuta, gesi asilia, misitu/wanyama pori na rasilimali uvuvi na kwamba jukumu la Serikali ni kuwezesha Wananchi wa maeneo husika kunufaika na umilikaji huo wa rasilimali asilia.

CHADEMA imetaka katiba mpya iwe na vifungu vya kuhakisha kuwa wananchi hawatanyang'anywa rasilimali zao asilia na mamlaka za Serikali matumizi na watu au taasisi nyingine ya rasilimali asilia za Wananchi bila kwanza Wananchi watakaoathiriwa na unyang'anyi au matumizi hayo kutoa ridhaa yao baada ya kupatiwa taarifa zote na kamili zinazohusu matumizi yanayotarajiwa ya rasilimali hizo na athari za matumizi hayo kwa mazingira, kiuchumi na kijamii (the right of prior informed consent).

Katiba mpya ihakikishe wananchi, Kama wamiliki wa msingi wa rasilimali asilia, watakuwa na haki ya kulipwa mrahaba kwa ajili ya matumizi ya watu au taasisi nyingine ya rasilimali asilia za Wananchi, wakati mamlaka za Serikali za mitaa, Majimbo na Serikali Kuu zitakuwa na haki ya kutoza kodi mapato yatakayotokana na matumizi ya rasilimali hizo.

Baraza Kuu limezingatia kuwa katiba ya sasa inatambua haki ya kumiliki mali na hifadhi ya mali hiyo na inakataza unyang'anyi wa mali kwa lengo la kuitaifisha au kwa malengo mengine, haki za wananchi kumiliki rasilimali zao za asilia kama ardhi, madini, mafuta, gesi asilia, misitu na wanyama pori, uvuvi, n.k., zimekuwa haziheshimiwi na mamlaka za kiserikali kwa hoja kwamba rasilimali asilia hizo ni mali ya umma.

Baraza Kuu limeelezwa kwamba dhana ya mali ya umma ni dhana yenye asili yake katika ukoloni. Ni dola ya kikoloni ya Kijerumani ndio ilikuwa ya kwanza kutangaza kwamba mali asilia zote katika koloni lao la Tanganyika ni mali ya Mfalme wa Kijerumani. Baada ya Wajerumani kushindwa Vita ya Kwanza ya Dunia na kunyang'anywa makoloni yao ya Afrika, dola ya kikoloni ya Waingereza iliyokabidhiwa Tanganyika, walitangaza kwamba rasilimali asilia zote ni mali ya umma chini ya mamlaka na udhibiti wa Gavana wa kikoloni. Dhana hii ilipokelewa bila mabadiliko yoyote ya msingi baada ya uhuru na ndio imekuwa msingi mkuu wa sera za rasilimali asilia za nchi yetu chini ya utawala wa Serikali inayoongozwa na CCM na kusababisha migogoro katika maeneo mengi nchini na kama ilivyo sasa huko Mtwara.

Kwa kuzingatia misingi hiyo, Baraza Kuu limeridhia msimamo wa Kamati Kuu kuhusu mgogoro wa gesi Mtwara kwamba tunataka wananchi wasikilizwe na serikali isimamishe mchakato wa kuvuna gesi ya Mtwara hadi itakapokuwa imetekeleza yafuatao: Iweke wazi mikataba yote ya utafutaji na uvunaji wa gesi ili wananchi wajue kama mikataba hiyo inalinda maslahi yao (ifahamike kwamba viongozi wa CCM na CCM kama chama kijinufaisha moja kwa moja na sehemu ya mikataba hiyo) ; waone jinsi wanavyonufaika na raslimali hiyo; Iweke wazi mikataba yote ya ujenzi wa bomba la gesi kutoka Mtwara hadi Dar es Salaam, ili wananchi wajue gesi hiyo inapelekwa wapi na kwa madhumuni gani; Ieleze kwanini haitaki kujenga vinu vya vya kufua umeme kwa kutumia gesi pale Mnazi Bay Mtwara, na kuingiza umeme wa 300 MW katika gridi ya taifa (CCM ijieleze kwa kushindwa kutekeleza ilani yake kuhusu ahadi hii) ; Iseme kwanini haiwezi kujenga mitambo ya kufua gesi Mtwara, na badala yake inang’ang’ania kujenga mabomba ya kupeleka gesi Bagamoyo na Dar es Salaam; na ieleze wananchi wa Mtwara na mikoa ya Kusini watafaidikaje na bomba linalopeleka gesi Bagamoyo.

Mapendekezo ya Haja ya kufanya marekebisho katika kanuni za chama na kutunga muongozo:



Baraza Kuu limefanya kwa mujibu wa mamlaka yake ya ibara ya 7.7.13 (i) ya kupokea mapendekezo na kuridhia haja ya kufanyia marekebisho ya kanuni za chama na kutunga muongozo.

Kati ya maeneo ya kanuni yaliyopendekezwa kufanyiwa marekebisho ni pamoja kuweka utaratibu wa wajibu na mipaka ya mbunge wa viti maalum kuondoa migongano na wabunge wa majimbo, kuweka utaratibu wa kuchukua hatua za kinadhamu mapema katika masuala yenye kuhitaji hatua za haraka kwa maslahi ya chama na taifa,  na mipaka ya wenza wa viongozi kwenye ushiriki wao katika shughuli za chama na nidhamu kuhusu muda wa mikutano.

Aidha, Baraza kuu limeridhia kuandaliwa kwa muongozo kuhusu utaratibu wa kutangaza kusudio la kugombea nafasi za uongozi kwenye chama na katika chaguzi za kiserikali kuanzia ngazi za kitongoji, kijiji/mtaa, udiwani, ubunge na urais.

Mpango Kazi, mwendelezo wa Operesheni ya M4C, ratiba ya uchaguzi na Bajeti ya chama ya 2013:

Baraza Kuu limepitisha Mpango Kazi, Mwendelezo wa Operesheni ya M4C, ratiba ya uchaguzi wa ndani wa chama na bajeti ya chama kwa mwaka 2013.

Baraza Kuu limezingatia kwamba matatizo yanayoikabili nchi kwa sasa ikiwemo migogoro mbalimbali na matokeo ya sera mbovu na udhaifu wa kiuongozi wa CCM na Serikali yake; hivyo CHADEMA kwa itaendelea kuwaongoza wananchi kuiwajibisha Serikali mwaka 2013, kueneza sera sahihi za CHADEMA na kuwaunganisha wananchi kuiondoa CCM madarakani katika chaguzi zinazokuja mwaka 2014 na 2015.

Kwa kuzingatia Ibara ya 3.A ya Katiba ya chama, Baraza Kuu limesisitiza falsafa ya chama ya “nguvu ya umma” katika kuongoza utekelezaji wa Mpango kazi kwa mwaka 2013 ya kwamba umma ndiyo wenye mamlaka ya mwanzo na mwisho katika kuamua hatma ya taifa na katika kumiliki na kuendeleza mawazo, maamuzi, rasilimali, uchumi na siasa za nchi.

Baraza Kuu limepitisha utaratibu wa mfumo wa utendaji wa kanda kwa kuzingatia misingi ya ‘sera ya majimbo’ na kwa kurejea katiba ya chama ibara ya 7.6 ili kugatua (decentralize) mfumo wa upangaji na utekelezaji wa shughuli za ujenzi wa chama kupitia operesheni za M4C.

Baraza Kuu limepitisha ratiba ya uchaguzi wa ndani ya chama ifuatayo: Uchaguzi wa misingi, matawi, majimbo na wilaya (Aprili mpaka Septemba 2013 kupitia Operesheni za M4C kwa kila kanda); Chaguzi za Mikoa (Novemba  2013); Uchaguzi  ngazi ya taifa ( Desemba 2013, Tarehe 11 BAWACHA, 12 BAVICHA na Wazee, 13 Kamati Kuu, 14 Baraza Kuu, 15 Mkutano Mkuu, 16 Baraza Kuu Jipya, 17 Kamati Kuu Mpya).
Imetolewa tarehe 29 Januari 2013 na:

John Mnyika (Mb)
Mkurugenzi wa Habari na Uenezi




No comments: