Hii ni
sehemu ya hotuba ya Kambi ya Upinzani Bungeni iliyosomwa na Kamanda Lissu
wakati wa Bunge la Bajeti Mei 3, 2013.
Ni ajabu
kuwa huyo huyo aliyetuhumiwa kwa ushahidi kuwa alikuwa anahujumu mchakato kwa
kushirikiana na wenzake wa CCM.
Uteuzi
katika wizara hii kama ilivyo katika wizara zote (esp' fedha, mambo ya ndani,
habari, mifugo, maji n.k), unahitaji Watanzania sote tufikirie sana kama
watawala hawa wanaitakia nchi hii mema.
Mheshimiwa
Spika
Kambi
Rasmi ya Upinzani Bungeni ina ushahidi unaoonyesha kwamba njama za kuhakikisha
kwamba wanaCCM pekee ndio watakaochaguliwa kuwa wajumbe wa Mabaraza ya Katiba
ya Wilaya kwa upande wa Tanzania Bara zilipangwa katika ngazi za juu kabisa za
CCM. Mnamo tarehe 3 Machi, 2013, siku mbili tu baada ya Mwongozo wa Tume kuanza
kutumika, Katibu wa NEC ya CCM, Uhusiano wa Kimataifa Dr. Asha-Rose Migiro
alituma barua pepe kwa wajumbe na watendaji wa Sekretarieti ya NEC ya CCM yenye
kichwa cha habari: ‘MUHIMU!! MABARAZA YA KATIBA YA WILAYA.’
Barua
pepe ya Dr. Asha-Rose Migiro inasema: “Naandika kuhimiza kazi ya kuwatia hamasa
Makatibu wa Mikoa wasimamie kikamilifu mchakato wa kuundwa kwa Mabaraza ya
Wilaya ya Katiba. Kama mnavyofahamu Tume ya Katiba imeshatoa taarifa rasmi
kwenye vyombo vya habari ... kuhusu zoezi hili muhimu. Sambamba na hatua za
awali tulizochukua baada ya kupata rasimu ya mwanzo ya Mwongozo wa Tume, hivi
sasa tunatakiwa tuongeze juhudi za ushiriki wetu na kutayarisha makundi husika
kama tulivyokwishaongea.”
Baada ya
kuagiza ‘mawasiliano kati ya SUKI na Makatibu wa Mikoa’ kuhusu mambo ya
kufanya, Dr. Asha-Rose Migiro alimalizia barua yake kwa maneno yafuatayo:
“Tafadhali wanakaliwa msisite kutoa maoni, ushauri na mbinu bora zaidi za
kutimiza azma yetu katika suala hili muhimu.” ‘Wanakiliwa’ wa barua pepe ya Dr.
Asha-Rose Migiro ni pamoja na Mh. Mwigulu Nchemba, Mh. Zakhia Meghji, Mh.
Muhamed Seif Khatib na Bw. Nape Nnauye, Katibu Mwenezi wa NEC ya CCM.
Siku
moja baadaye, Nape Nnauye aliwaandikia ‘wanakiliwa’ wenzake kama ifuatavyo:
“NASHAURI ikiwezekana kwa sababu ya unyeti wa swala hili tupate taarifa kila
siku/au walau siku tatu ya HALI HALISI inavyoendelea katika kila mkoa, ni
vizuri idara ikaandaa checklist ya mambo muhimu ya kupima kama mchakato
unakwenda vizuri au la! Mfano ... idadi ya walioandaliwa kugombea katika kila
eneo, idadi ya waliohamasishwa kuhudhuria na kupiga kura, n.k.”
Mheshimiwa
Spika,
Njama za
CCM kuteka nyara mchakato wa Katiba Mpya zinahusu pia mchakato wa uhalalishaji
wa Katiba Mpya kwenye kura ya maoni. Mnamo tarehe 18 Desemba mwaka jana, Katibu
wa Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM, Francis K. Mwonga,
aliwaandikia barua Makatibu wote wa CCM wa Mikoa kuwapa ‘Maelekezo ya Kikao cha
Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya Taifa na Makatibu wa CCM wa Mikoa
Kilichofanyika Dar es Salaam Tarehe 10/12/2012.’
Sehemu
ya Maelekezo hayo inasema: “Wakati wa kupiga kura ya maoni kuhusu Katiba Mpya
ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mawasiliano yafanywe na wahusika ili vituo
vya kupigia kura visiwe mbali sana na wananchi.” Maneno haya yameandikwa hata
kabla Tume haijamaliza zoezi la kukusanya maoni ya wananchi na tayari
Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya CCM inawaelekeza makada wake mikoani kufanya
mawasiliano na ‘wahusika’ juu ya namna ya kupanga vituo vya kupigia kura.
Mheshimiwa
Spika,
Kwa
mujibu wa kifungu cha 56(a) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, Sura ya 343 ya
Sheria za Tanzania, mamlaka inayohusika kupanga vituo vya kupigia kura ni
Msimamizi wa Uchaguzi, yaani Mkurugenzi wa Jiji, Mkurugenzi wa Manispaa,
Mkurugenzi wa Mji na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya. Wasimamizi
hawa wa uchaguzi wamelalamikiwa kwa miaka mingi na vyama vya upinzani kwa
kupendelea CCM na wagombea wake katika chaguzi mbali mbali. Hawa ndio wanaotakiwa
wawasiliane na Makatibu wa CCM Mikoa ili wapange vituo vya kupigia kura ya
maoni juu ya Katiba Mpya!
Mheshimiwa
Spika,
Mawasiliano
haya ya viongozi wa ngazi za juu za CCM yanathibitisha kwamba mchakato wa
Katiba Mpya umeiingiliwa na kuhujumiwa kwa kiasi kikubwa na CCM.
Aidha,
mawasiliano haya yanathibitisha kauli iliyotolewa mbele ya Bunge lako tukufu na
Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni wakati wa mjadala wa hoja ya Ofisi
ya Waziri Mkuu kwamba “...viongozi wa kiserikali kama vile Wakuu wa Wilaya na
wa Mikoa waliwahamasisha wenyeviti wa vijiji, mitaa na madiwani kuhakikisha
kwamba wagombea wote wasiokuwa wa CCM, hasa wa CHADEMA, wanaenguliwa katika
chaguzi za vijiji, mitaa au kata.” Aidha, mawasiliano haya yanathibitisha kauli
ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kwamba Mabaraza ya Katiba ya Wilaya
yaliyochaguliwa kwa utaratibu “...ni mabaraza ya CCM na sio mabaraza ya katiba
ya Watanzania wote.”.
1 comment:
Mimi nashauri baada ya kugundua mbinu wanayotumia ccm, Chadema nayo itumie mbinu hizohizo ili mradi polisi wasihusishwe
Post a Comment