Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora

Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora
----------------------WE THANK AND APPRECIATE YOU FOR VISITING CHADEMA DIASPORA BLOG. AGAIN, THANK YOU!-----------------------

Wednesday, July 17, 2013

Ndugai aigeuka CCM

Amgeuka pia Makinda, asema ni uongo, unafiki kupinga Serikali tatu

     WAKATI Chama Cha Mapinduzi (CCM), kikipinga mapendekezo ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba Mpya juu ya muundo wa Muungano wa Serikali tatu, kiongozi wake ambaye ni Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai amekigeuka chama hicho akisema kuwa wanaopinga suala hilo waache unafiki, uongo na kudanganyana. Ndugai ambaye kwa upande wake alisema anaunga mkono muundo wa Serikali tatu kama Rasimu ya Katiba mpya inavyopendekeza, alitoa msimamo wake huo juzi wakati akizungumza kwenye kipindi cha ‘Dakika 45’ kinachorushwa na kituo cha televisheni cha ITV.  Alisema kulingana na maoni yaliyotolewa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, ameyapokea kwa mikono miwili, hivyo wananchi wanatakiwa kuisoma rasimu hiyo na wasiisome kama gazeti.

   “Lakini moja ya mjadala mkubwa ni Serikali tatu, sio siri watu wamekuwa wakilijadili sana na hasa kutoka upande wa visiwani, ni jambo ambalo wazee wetu wameliweka uwanjani tulitazame, na tunapaswa kulitazama kwa umakini kwa sababu hili ni suala la msingi sana katika uendeshaji wa nchi yetu. “Ninadhani tuache unafiki, uongo na kudanganyana kwa hali ilivyo huwezi kuzungumzia serikali moja au mbili wenzetu Zanzibar watajiona wamemezwa, hili ni jambo ambalo lilishindikana tangu mwaka 1964, ni kero ambazo hata ufanye nini zitaendelea, kwa hiyo nadhani wazee hawa walifikiri sana na nadhani wako sahihi kabisa,” alisema Ndugai ambaye pia ni Mbunge wa Kongwa kupitia CCM.  Alisema suala la kutengana kwa sasa halipaswi kuzungumziwa labda huko baadaye, kwani suala la msingi sasa ni kuwasikiliza Wazanzibari wanataka nini na sio kuendeleza kiburi.


    Mchakato wa Katiba mpya ya Tanzania upo katika hatua ya rasimu na watu mbalimbali kupitia Mabaraza ya Katiba, wameanza kutoa maoni yao.  Tayari CCM kupitia Kamati Kuu yake iliyoketi mjini Dodoma mwishoni mwa mwezi uliopita, kiliweka msimamo wa kutaka kuwepo kwa mfumo wa Serikali mbili katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete amekwishatangaza kuwa chama hicho kitakuwa moja ya mabaraza ya Katiba na kupata nafasi ya kuichambua, kuijadili na kutoa maoni kuhusu rasimu iliyotolewa hivi karibuni na Tume ya Mabadiliko ya Katiba chini ya mwenyekiti wake Jaji mstaafu Joseph Warioba.

     Wakati CCM kikiweka msimamo wake huo, Chadema kwa upande wake kimeeleza bayana kuunga mkono Serikali tatu, kama anavyopendekeza Ndugai. Vyama vingine kama CUF, msimamo wake umekuwa haueleweki, kwa sababu wakati Mwenyekiti wake, Profesa Ibrahimu Lipumba akiunga mkono Serikali tatu, Katibu Mkuu wa chama hicho, Maalim Seif anataka iwepo Serikali ya Mkataba.

AMPINGA MAKINDA

      Mbali na hilo la Serikali tatu, Ndugai pia alimgeuka Mkuu wake wa kazi Spika Anne Makinda, kwa kupinga mapendekezo aliyoyatoa kwamba, Katiba mpya ijayo isiruhusu viongozi wanaoshika nafasi hizo za Spika na Naibu Spika kuwa wanachama wa chama chochote cha siasa. Akizungumzia muundo wa Bunge la Jamhuri, Ndugai alisema kulingana na mapendekezo yaliyotolewa kwenye rasimu hiyo, inaonesha wanataka kuondoa mgongano wa vyama vya siasa ndani ya mhimili huo, jambo ambalo ni gumu sana. “Unapopewa uongozi, unaapishwa kutenda haki, utakapoanza kutafuta sijui mtu hana chama sijui hayupo hivi au hivi ni sawa sawa na kusema kwamba sasa Tanzania tuna migongano ya kidini ya Ukristo na Uislamu, kwa hiyo tunadhamiria kutafuta Rais ambaye sio Mkristu wala Muislamu. 

     “Sijui kama itakuwa ndiyo lengo, tunachotaka Rais wetu asitubague kidini, tutampata Rais au Spika kwa vyovyote vile atakuwa mpenzi au mwanachama shabiki wa chama fulani, lakini tutakapompa nafasi yetu ya uspika au naibu spika au uongozi wa chombo kile cha mhimili atende haki, huo ndio mtihani,” alisema. Alisisitiza kuwa kutafuta watu ambao hawana chama, kwa mawazo yake sio sawa kwani inawezekana kabisa kukawepo na watu waliopewa nafasi hizo bila na kutekeleza majukumu yake bila ubaguzi.  Kuhusu suala la mgombea binafsi, Ndugai alisema hilo ni jambo ambalo halipingiki kwa sasa.

     “Jambo la msingi niwakumbushe wabunge kuwa Bunge la Katiba litaanza Novemba, Desemba na Januari, hivyo natoa wito kwa wabunge tusilete ushabiki wa vyama, Utanganyika wala Uzanzibari, tutengeneze Katiba nzuri kwa miaka mingi ijayo, nchi yoyote yenye maendeleo misingi yake ni Katiba,” alisema. Msimamo huo wa Ndugai unakuja ikiwa ni miezi michache imepita tangu Spika wa Bunge Anne Makinda atoe maoni ya ofisi yake kuhusu muundo wa bunge inaolipendekeza na kutaka Spika na Naibu Spika au viongozi wengine wa Bunge, wasitokane na vyama vya siasa ili kuepusha mgongano unaojitokeza mara kwa mara ndani ya Bunge na malalamiko yanayotolewa dhidi ya ofisi yake kuhusu kupendelea chama tawala.

Source: Mushi G. (July 2013). Ndugai aigeuka CCM. Retrieved from Mtanzania

No comments: