ATAKA UBABE WAKE UDHIBITIWE NA GEORGE MAZIKU NA ASHA BANI
Dk. Slaa alibainisha kuwa hulka ya chama tawala nchini kutegemea
mabavu kuongoza nchi inatokana na chama hicho kudumu madarakani kwa zaidi ya
miaka 27 peke yake bila kuwepo vyama vya upinzani. Alisema kipindi hicho
kirefu ambacho CCM ilitawala bila kuwepo upinzani iliwafanya viongozi wake
waamini kuwa wanayo haki ya kuitawala Tanzania peke yao. “Kama
inavyoeleweka kuwa madaraka hulevya, madaraka makubwa kupindukia hulevya zaidi.
Viongozi wetu waliamini katika matumizi ya madaraka ya kisiasa ili kudumisha
utawala wao. Waliwatazama wapinzani wote kwa ghadhabu bila kujua kuwa ghadhabu
ni jambo la hatari,” alisisitiza. Alisema kuwa kwa sasa CHADEMA inaandamwa
vikali na taasisi mbili za kiserikali ambazo ni Msajili wa Vyama vya Siasa na
Jeshi la Polisi.
Aliongeza kuwa msajili amekuwa akitishia kukifuta chama hicho huku
polisi wakiwaandama viongozi na wanachama wa CHADEMA, na watu wengine wote
wanaojitokeza kuwatetea. Alibainisha kuwa hali hiyo inatokana na tangazo
la hivi karibuni la chama chake kwamba kinaanzisha mafunzo ya ukakamavu kwa
vijana wake ili waweze kutoa ulinzi kwa viongozi wao na mali za chama
hicho. Alisema kuwa pamoja na kwamba mafunzo hayo yamo katika katiba ya
chama chao iliyosajiliwa na msajili wa vyama vya siasa, na pia kuruhusiwa na
sheria za nchi, amekuwa akidai mafunzo hayo yanakiuka sheria na kutishia kukifuta. Aliongeza
kuwa wakati msajili akitishia kuifuta CHADEMA, polisi wamekuwa wakiendeleza
harakati za vitisho vya kuwakamata na kuwashtaki.
Dk. Slaa alisema matukio ya siku za karibuni ya polisi kuzidi
kuwaandama viongozi wao na kufikia kuwavamia majumbani wakiwa na silaha nzito,
yamezidi kuwatia woga. Hata hivyo, Dk. Slaa alisema kuwa vikwazo
vinavyowekwa na CCM dhidi yao ni ufunguo wa kufikia malengo yao ya kuwapatia
wananchi nguvu ili wazitumie nguvu hizo kuilazimisha serikali yoyote kuwajibika
kwao kwa kutekeleza matakwa yao. “Mafanikio makubwa yanahitaji ukakamavu.
Tuna haki kama chama kilichosajiliwa kisheria kujilinda sisi na mali zetu,”
alisisiza Dk. Slaa.
Source: Tanzania Daima ( July 2013).
Dk. Slaa awavaa CCM. Retrieved from Tanzania Daima
No comments:
Post a Comment