Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora

Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora
----------------------WE THANK AND APPRECIATE YOU FOR VISITING CHADEMA DIASPORA BLOG. AGAIN, THANK YOU!-----------------------

Tuesday, July 23, 2013

CHADEMA, CCM wavutana vikali

MJADALA WA SERIKALI TATU



    CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimesema Muungano wa serikali mbili za sasa unatumia gharama kubwa kuliko serikali tatu zinazopendekezwa karika rasimu ya Katiba Mpya. Kimesema hoja ya Chama cha Mapinduzi (CCM) kupinga shirikisho la serikali tatu kwa kigezo cha ukubwa wa gharama ni potofu kwa sababu mfumo unaopendekezwa utapunguza utitiri wa vyeo na kudhibiti matumizi yasiyo ya lazima. Tanzania Daima imeona andishi la CHADEMA linalotarajiwa kuzinduliwa wakati wowote kuanzia sasa, ambalo ndiyo msimamo rasmi wa chama hicho kuhusu rasimu ya Katiba Mpya. Miongoni mwa mambo mengi yanayochambuliwa kwa vielelezo ni hoja ya serikali, ambayo CCM imekuwa inahamasisha wanachama wake waikatae, na badala yake wapendekeze serikali mbili za sasa kwenye mabaraza ya katiba yanayoendelea.

CHADEMA imesema kuwa madai ya CCM kuwa serikali ni mzigo kwa taifa, hayana ukweli kwani serikali mbili za sasa zinatafuna mabilioni ya shilingi ambayo yataokolewa iwapo serikali zitakuwa tatu. Katika kifungu cha ukubwa wa serikali, CHADEMA imesema kwa muundo wa sasa wa serikali mbili, kuna viongozi wakuu sita (6), wakati mfumo wa serikali tatu utakuwa na viongozi wasiozidi wanne (4). Imesema wabunge na wawakilishi 438, huku katika serikali tatu kutakuwa na wabunge wasiozidi 314.
Kwamba pamoja na hesabu hii, bado upo uwezekano wa idadi hii kupungua zaidi kwa kuwa mchakato wa kuandika Katiba ya Tanganyika na marekebisho/mabadiliko ya Katiba ya Zanzibar kutokana na mabadiliko ya muundo wa Muungano unaweza kuja na mifumo tofauti ya uwakilishi au mgawanyo wa majimbo mapya ya uchaguzi.

       “Bunge la Jamhuri ya Muungano la sasa lina idadi ya wabunge 357, ukitoa wabunge 189 wa majimbo ya uchaguzi ya Tanzania bara na 50 ya Zanzibar; 102 wa viti maalumu na 10 wa kuteuliwa na rais, watano wanaowakilisha Baraza la Wawakilishi Zanzibar na Mwanasheria Mkuu. “Kwa upande wa Baraza la Wawakilishi kuna jumla ya wawakilishi 81-50 wanaowakilisha majimbo ya uchaguzi, 10 wa kuteuliwa na Rais wa Zanzibar, 20 wa viti maalumu, na mwanasheria Mkuu wa Zanzibar, kwa maana hiyo kwa muundo wa sasa wa Muungano, mabunge mawili tuliyonayo yana idadi ya wabunge 438. “Idadi hiyo ni kubwa kuliko idadi ya wabunge wa mabunge matatu yatakayokuwepo chini ya muundo wa serikali tatu kwa wabunge 124,” imesema CHADEMA.

      Ukweli huu unaiweka pabaya CCM ambao walidai kuwa serikali tatu inayopendekezwa na tume na kuungwa mkono na wapinzani itakomba fedha nyingi za Watanzania. “Mapendekezo ambayo ndiyo msimamo wa chama tulishayawasilisha kwenye tume kuwa sisi tunapendekeza mfumo wa serikali mbili na siyo tatu wala moja,” alisema Nape alipokuwa akitoa taarifa ya uamuzi wa Kamati Kuu (CC) ya CCM iliyokutana usiku wa kuamkia jana kujadili suala hilo. Kauli ya Nape inafanana na matamshi ambayo yamewahi kutolewa na baadhi ya wanasiasa wakongwe ambao ni makada wa CCM, wakiwamo mawaziri wakuu wastaafu, Frederick Sumaye na John Malecela, Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta na baadhi ya wabunge ambao mara kadhaa wamekaririwa wakipinga pendekezo la serikali tatu.

      Hata hivyo, wabunge wa Zanzibar, akiwemo Mbunge wa Uzini, Mohamedi Seif Khatibu na Mjumbe wa Kamati ya Halmashauri Kuu ya CCM, Balozi Seif Idd, walisema watu watakaopinga serikali mbili wafukuzwe Chama Cha Mapinduzi. Ifuatayo ni sehemu ya msimamo wa CHADEMA kuhusiana na uendeshaji wa serikali tatu: Kwanza, hadi sasa hakuna mtu yeyote au taasisi yoyote iliyofanya uchambuzi wa uangalifu wa gharama za kuendeshea serikali, iwe moja, mbili au tatu katika nchi yetu. Kwa sababu hiyo, hakuna ushahidi wowote wa kuthibitisha kwamba kuendesha serikali tatu ni ghali zaidi kuliko kuendesha serikali mbili. Pili, Kama suala la gharama za kuendeshea serikali ndio jambo muhimu zaidi katika kuamua muungo wa Muungano, wanaopinga shirikisho la serikali tatu wangeeleweka kama wangependekeza muundo wa serikali moja tu, badala ya serikali mbili za sasa wanazoziunga mkono, au hata tatu zinazopendekezwa na rasimu.

     Tatu, kama mapendekezo ya rasimu juu ya mambo ya Muungano yakichukuliwa kuwa kigezo cha kupima ukubwa wa serikali na gharama za kuiendesha, basi gharama za serikali ya Muungano zinaweza kuwa ndogo sana. Nne, kama mambo saba ya Muungano yanayopendekezwa na rasimu, hakutakuwa na zaidi ya wizara nne za Serikali ya Muungano. Hivyo kwa mfano kutakuwa na Wizara ya Katiba na Sheria itakayoshughulikia masuala ya katiba na mamlaka ya Jamhuri ya Muungano; Wizara ya Ulinzi itakayokuwa na majukumu ya ulinzi na usalama wa Jamhuri ya Muungano na Wizara ya Fedha itakayoshughulikia masuala ya sarafu, Benki Kuu na ushuru wa bidhaa na mapato yatokanayo na mambo ya Muungano, na Wizara ya Mambo ya Nje.

      Masuala yaliyobaki yaani uraia na uhamiaji na usajili wa vyama vya siasa hayastahili kuwa na wizara zinazojitegemea, kwa hiyo yanaweza kuwekwa chini ya wizara zilizotajwa. Aidha aya ya 93(2) ya rasimu inapendekeza ukubwa wa Baraza la Mawaziri wasiozidi kumi na tano. Hata hivyo aya ya 93(3) inaelekeza kwamba Serikali ya Jamhuri ya Muungano itakuwa na wizara kwa kuzingatia mamlaka ya serikali kwa mujibu wa katiba hii, kwa namna nyingine ukubwa wa serikali lazima uzingatie mambo saba ya Muungano. Kwa sababu hiyo Serikali ya Jamhuri ya Muungano haiwezi kuwa na mawaziri wengi kuliko mambo saba ya Muungano.

      Kwa mtazamo huo huo, aya 93(3) na orodha ya mambo ya Muungano kama kipimo cha ukubwa wa Srikali ya Muungano haiwezekani katibu mkuu kiongozi na makatibu wakuu wanaopendekezwa katika aya za 98 na 99 za rasimu kuwa zaidi ya wanne. Kwa kuzingatia idadi ya makatibu wakuu wenyewe, kamati maalumu ya makatibu wakuu inayoelekezwa katika aya ya 100 na Sekretarieti ya Baraza la Mawaziri inayotarajiwa katika aya ya 101 hazina maana wala umuhimu wowote kikatiba. Kwa kuzingatia mapendekezo ya rasimu kuhusu Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika aya ya 105, kwa idadi ya sasa ya mikoa ya Tanzania bara na wilaya za Zanzibar, Bunge la Jamhuri ya Muungano litakuwa na wabunge 75 kwa mapendekezo ya muundo wa serikali tatu, endapo Bunge la Zanzibar litakuwa na wabunge 50 wa majimbo ya sasa ya uchaguzi.

     Kwa maana hiyo muundo wa Muungano wa serikali tatu utakuwa na mabunge matatu yenye jumla ya wabunge 314. Upo uwezekano wa idadi hii kupungua zaidi kwa kuwa mchakato wa kuandika katiba ya Tanganyika na marekebisho/mabadiliko ya Katiba ya Zanzibar kutokana na mabadiliko ya muundo wa Muungano unaweza kuja na mifumo tofauti ya uwakilishi au mgawanyo wa majimbo mapya ya uchaguzi. Kwa kulinganisha Bunge la Jamhuri ya Muungano la sasa lina idadi ya wabunge 357, ukitoa wabunge 189 wa majimbo ya uchaguzi ya Tanzania bara na 50 ya Zanzibar; 102 wa viti maalumu na 10 wa kuteuliwa na rais, watano wanaowakilisha Baraza la Wawakilishi Zanzibar na Mwanasheria Mkuu.

     Kwa upande wa Baraza la Wawakilishi kuna jumla ya wawakilishi 81-50 wanaowakilisha majimbo ya uchaguzi, 10 wa kuteuliwa na Rais wa Zanzibar, 20 wa viti maalumu, na Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar, kwa maana hiyo kwa muundo wa sasa wa Muungano, mabunge mawili tuliyonayo yana idadi ya wabunge 438. Idadi hiyo ni kubwa kuliko idadi ya wabunge wa mabunge matatu yatakayokuwepo chini ya muundo wa serikali tatu kwa wabunge 124! Taasisi nyingine za Muungano zinazopendekezwa kama vile Tume ya Mahusiano na Uratibu wa Serikali, na Tume ya Utumishi wa Umma haziwezi kuwa kubwa sana kwa kuzingatia ukubwa wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano kwa mujibu wa rasimu. Taasisi nyingine kama vile Tume ya Maadili ya Uongozi na Uwajibikaji, Tume ya Haki za Binadamu hazipo kwenye orodha ya mambo ya Muungano na uwepo wao kwenye rasimu unakinzana na matakwa ya aya za 59 na 60 za rasimu.

      Kama majukumu ya taasisi hizo hayahusu mambo ya Muungano, tume haziwezi kugharamiwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano. Hata hivyo baada ya kukubalika kwa pendekezo la kuyaingiza masulala hayo katika orodha ya mambo ya Muungano, bado gharama zinaweza kupunguzwa kwa kuweka mfumo wa utekelezaji wa taasisi husika kupitia makubaliano na washirika wa Muungano. Majukumu ya utekelezaji wa mambo mengine ya Muungano kama uchaguzi na usajili wa vyama vya siasa yanaweza kutekelezwa na taasisi husika za washirka wa Muungano kwa makubaliano na masharti maalumu chini ya aya ya 59(3) ya rasimu. Hii nayo itapunguza gharama za kuendesha Serikali ya Jamhuri ya Muungano.

Source: Tanzania Daima ( July 2013). CHADEMA, CCM wavutana vikali. Retrieved from Tanzania Daima

No comments: