Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora

Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora
----------------------WE THANK AND APPRECIATE YOU FOR VISITING CHADEMA DIASPORA BLOG. AGAIN, THANK YOU!-----------------------

Wednesday, June 19, 2013

CHADEMA haiwezi kushindana na serikali kwa namna hii; Iitishe mgomo wa Kitaifa!

M. M. Mwanakijiji

Kilichotokea Arusha Jumamosi iliyopitajioni ni kitu cha kulaaniwa kwa kauli yote kali. Lakin pia ni kitu ambacho kinahitaji CHADEMA ioneshe kuwa ‘sasa imetosha’. Inawezekana vipi ndani ya miaka karibu mitatu tu vitendo vya kinyama vimekuwa vikifanyika dhidi ya Wanachadema mara kwa mara wanapojaribu kufanya mikutano ya amani? Ni nani amesahau yaliyotokea ile Januari 5 huko huko Arusha na matukio mengine yaliyofuatia kuanzia Mwanza, Iringa, Morogoro, Songea, Tukuyu, Mbeya, Igunga na sehemu nyingine?

Hivi ni kweli nchi yetu ina vyombo vyovyote vya usalama? Ni kitu gani kwa kweli wameweza kukilinda kikawa salama? Matukio haya yote yangelazimisha kufukuzwa kwa watendaji wakuu wa vyombo vya usalama – Polisi, TISS n.k. Nilishawahi kuuliza huko nyuma katika mojawapo ya makala zangu – MPAKA NANI AUAWE ndio tutajua kuwa tuna tatizo?

Tukio la Arusha ni ishara tu ya kile ambacho kiko vibaya – ubovu wa mfumo wetu wa intelligensia na usalama. Kama tunavyojua tukio hili limekuja miezi michache tu baada ya tukio kama hilo huko huko Arusha katika Ibada ya Wakfu ya Kanisa Katoliki. Nani atasahau mazingira yale ni kama yamejirudia tena? Na safari hii sijui watamkamata kijana gani maana hawa vijana wenye ujuzi na uthubutu wa hivi ni lazima wawe makini kweli – na inaonekana wako wengi! Yule mwingine bado yuko ndani halafu kuna mwingine/wengine?

CHADEMA ndio wamekuwa waathirika wakuu wa matukio haya nan i wanachama na viongozi wao ambao wamekuwa wakifanyiwa vitendo vya aina hii na inashangaza wakati mwingine mbele ya polisi. Ni nani amesahau jinsi wale wabunge wa CDM walivyopigwa kule Mwanza? Au nani kasahau watendaji wa CDM walivyopigwa kule Kiteto? Au nani kasahau mauaji ya kinyama ambayo Polisi hadi leo hawayajtolea maelezo ya kijana wa CDM kule Igunga? Au ni kumbushe tukio lile la Januari 5 huko huko Arusha?

Bahati mbaya sana CDM bado wameendelea kuamini kuwa kwa kudra za Mwenyezi Mungu jeshi la polisi litabadilika sasa hivi na kuonesha weledi na kutoa ulinzi na kuhakikisha usalama wao. Wapo kabisa watu ndani ya CDM wanaoamini kuwa wakitoa kauli kali basi Polisi watetemeka au kina Mwema watabadilika? Ni ndoto za Alinacha. Bila kuwatumia ujumbe watawala kuwa mizani ya nguvu imebadilika na sasa upepo umebadilika. Maneno makali na nyuso za huzuni na hata machozi havijawatisha watawala na zaidi tumeona kuwa vinawafanya wawe na mioyo migumu zaidi! Inahitaji moyo sana kulaumu wahanga kwa madhara yanayowapata!

Maoni yangu yako wazi kabisa CDM waoneshe msimamo vinginevyo – na nilishawahi kuwaambia ndugu zangu hawa – wataendelea kuzika na kubeba majeneza ya wanachama wao na mashabiki wao. Msimamo wao uwe wazi kabisa kuwa sasa imetosha. Baadhi ya mambo ambayo naamini yanatakiwa yawepo kwenye msimamo huo:

a. Kutaka Mkuu wa Jeshi la Polisi na Mkuu wa Operesheni pamoja na DCI kujiuzulu au kufukuzwa kazi. Matukio kama haya yanahitaji watu kuwajibishwa siyo kupandishwa vyeo kama ilivyotokea kwa Kamuhanda!

b. Kutaka Mkuu wa Usalama wa Taifa awajibishwe. Taasisi hii imekuwa dhaifu kuliko wakati wowote wa historia yetu. Udhaifu wake unatokana kwa kiasi kikubwa na kuwa “compromised”. Inapofikia mtumishi wa Idara anakufa kwenye kisima cha maji Makao Makuu ya Idara pamoja na mauaji na vifo vya baadhi ya maafisa wa TISS ndani ya miaka miwili tu inatosha kuhoji weledi, uwezo, na utendaji wa Mkurugenzi wa Idara hiyo.

c. Kutaka Waziri wa Mambo ya Ndani awajibike au awajibishwe. Ameshindwa kuonesha uongozi na maono ya kulibadilisha jeshi la polisi kulifanya liwe la kisasa na siyo la kisiasa kama lilivyo sasa.

e. Msajili wa Vyama vya Siasa John Tendwa awajibike yeye mwenyewe kwa kuvumilia kauli za viongozi wa CCM ambao kwa kauli zao wao wenyewe wamejithibitisha kuwa wako katika mipango ya kukidhulumu Chama cha Demokrasia na Maendeleo. Msajili anaposhindwa kukemea na kuwawajibisha watendaji hawa anaonekana kukibeba na tusije kushangaa na yeye akimaliza zamu yake atapozwa na ka-jiubalozi fulani ‘somewhere’.

Kilichotokea ni mwendelezo wa kuvurugika na kubomoka kwa mfumo wa Usalama na Intelligensia wa Tanzania; ni matokeo ya kuendekeza mifumo ya usalama ambayo imeshaonesha kuwa imeshindwa. Kama watu wanaweza kufanya hivi kwa uchaguzi wao – iwe kanisani au uwanjani- hivi tumefikiria uwezekano wa jambo kama hili kutokea mahali ambapo pana viongozi wa serikali, watoto, au mashuleni? Ni udhaifu gani huu wa mfumo?

Sasa yasiwe matakwa ya juu juu tu; ujio wa Rais Obama ni nafasi nzuri ya kusukumikiza ajenda ya haki za kiraia na binadamu nchini na mbele ya jamii ya Kimataifa. Njia mojawapo ni kutumia nafasi ya ujio huu kuitisha maandamano makubwa zaidi nchini yawe ya active (ya watu kuandamana) au ‘passive’ ya kusimamisha shughuli zote nchini dhidi ya Jeshi la Polisi na Serikali endapo watajwa hapo juu hawatakuwa wameondolewa.

Si lazima kufanya maandamano ya watu kutembea barabarani kwani kufanya hivyo ni kuwapa kisingizio watawala kutumia nguvu zaidi; lakini inawezekana pia kufanya maandamano ya kunyamaza; aina ya mgomo wa kuwakatalia watawala. Yaani, kukataa kufanya mambo fulani ambayo yatatuma ujumbe kwa watawala kuwa sasa “nguvu ya umma” imechoka na itatumika.

Watanzania na wapenda mabadiliko wanasubiri kuona CDM itafanya nini tena; je itaendelea kutoa maneno makali na kuendelea kucheza ‘zero distance’ na CCM huku wanachama wake wakiendelea kupopolewa na damu kumwagika? Je wataendelea kukubali kubebeshwa lawama kwa matukio ambayo yanawaangukia wao?

Kama CDM wanaona kuwa hawawezi kufanya passive resistance kama ambavyo kina Martin Luther Kinga walifanya na kusababisha mabadiliko basi wasitishe maandamano na mikutano yao. Haiwezekani waendelee kufanya mikutano na watu wao wanapigwa na kuumizwa halafu wanaishia kutoa matamko makali na sura zilizojaa ndita lakini wakija kwenye vitendo hakuna kinachofuatia! Siyo tu kusitisha maandamano bali watangaze kutokushiriki uchaguzi mwingine wowote kwani gharama ya kufanya chaguzi hizi ni kubwa zaidi kwa maisha ya watu kuliko watu wanavyofikiria.

Binafsi nitalaani vikali kama CDM itashiriki uchaguzi wa marudio hapo Arusha kama watu wale wale – Polisi, Usalama wa Taifa, RPC na Msajili wa vyama wataendelea kuwepo. NItalaani kwa sababu CDM itakuwa inakubali kuwa chini ya huruma ya watu wale wale waliothibitika kushindwa na walioonesha udhaifu uliopitiliza. Vinginevyo, watakuwa wanakejeli damu ya MASHAHIDI WA TANZANIA MPYA ambayo tayari imemwaga nchini!

Ni kwa hili tu nitaendelea kuwaunga mkono CDM badala ya kusubiri kauli za kisiasa na kunyemeleana. Wanachama na Mashabiki wenu wanataka kuona mnaongoza siyo mnavaa magwanda lakini hamuoneshi uthubutu wa kusimamia mnachoamini. Magwanda na kauli kali wakati wa mazishi mengine hazitoshi tena. Ni wakati wa vitendo. Na hapa simaanishi vitendo vya kulipiza kisasi; bali vitendo vitakavyomulika udhaifu wa vyombo vya usalama lakini zaidi vitendo vitakavyomulika jinsi haki za raia na haki za binadamu zinavunjwa nchini.

Na hili linaweza kufanywa kwa kuitisha mgomo wa kitaifa kama aina ya passive resistance ya utawala wa kiimla wa chama kimoja. Siku hii siyo tu ya watu kugoma kwenda kazini lakini pia kufunga, na kufanya mambo yaende pole pole (go slow movement). Mfano mzuri wa hii go slow ni kama kilichotokea hapa Detroit miezi michache nyuma ambapo wananchi wanaotumia magari waliamua kupunguza mwendo kwenye barabara kuu kupinga kitendo cha Serikali ya Jimbo kumteua Mwangalizi Maalum wa Jiji na kuwaweka pembeni viongozi wa kuchaguliwa wa Jiji hili lenye matatizo. Japo Mwangalizi huyo aliweza kuja lakini hakuweza kufanya mengi bila kuwahusisha viongozi kwani wananchi walishaonesha namna ya kugoma. Unapotumia ‘passive resistance’ polisi na usalama wa taifa hawana cha kufanya! Hawawezi kuwalazimisha watu kutembea haraka au kwenda kazini! 

Hili lisiwe kwa watu wengine tu bali wabunge wote wa CDM nao wagome kuingia Bungeni kwa muda wote wa siku za mgomo (na hivyo kunyimwa posho za siku hizo). Ujumbe ni lazima utumwe kuwa nguvu ya umma ni kweli ina nguvu. Nguvu ya umma isiwe katika kuhesabu umati wakati wa kuhutubia au maandamano; bali iwe katika kulazimisha serikali kufanya mabadiliko.

Facebook:"Mzee Mwanakijiji"


No comments: