Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora

Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora
----------------------WE THANK AND APPRECIATE YOU FOR VISITING CHADEMA DIASPORA BLOG. AGAIN, THANK YOU!-----------------------

Thursday, May 23, 2013

"Vita" Mtwara

Polisi wapambana na wananchi kila kona

Gari la maji ya kuwasha lachomwa, nyumba

Madaraja muhimu yavunjwa, shule zafungwa



VURUGU kubwa zimeibuka tena mkoani Mtwara jana na kulazimisha Jeshi la Polisi kutumia risasi za moto, mabomu ya machozi na kila aina ya mbinu, kupambana na wananchi wanaopinga kitendo cha Serikali kutaka kusafirisha gesi kwenda Dar es Salaam. Taarifa kutoka Mtwara, zinasema hadi jana jioni kulikuwa na uharibifu mkubwa wa miundombinu na uchomaji wa nyumba za watumishi wa Serikali na viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Mbali ya matukio hayo, inadaiwa kulikuwa na mauaji ya askari polisi kadhaa, huku wananchi wengi wakitiwa mbaroni kutokana na vurugu hizo. Chanzo cha vurugu hizo, kinadaiwa kilitokana na hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini kusomwa Bungeni na Waziri Sospeter Muhongo, ambapo alisisitiza mradi wa gesi wa Mtwara utatekelezwa bila kutaja faida za moja kwa moja kwa wananchi hao. Wananchi hao, walianzisha vurugu jana, huku wakiwa na kauli mbiu yao isemayo "Gesi haitoki hata kwa bomba la peni". Inaelezwa kuwa kuna kituo cha mafuta cha Total kimechomwa moto wakati wa vurugu hizo.


Taarifa zinasema katika eneo la Mikindani ofisi zote za serikali, zilivamiwa na kuchomwa, likiwamo daraja la Mikindani. Katika eneo hilo ambako kuna daraja maarufu la Mikindani, lilivunjwa, baada ya kulipuliwa na kitu kinachosadikiwa kuwa bomu. Kutokana na hali hiyo, askari wanafanya msako wa nyumba hadi nyumba maeneo ya Magomeni na Mangowela.  “Hali ni mbaya mno, polisi wamelazimika kutumia helkopita kupita maeneo yote ya mjini, hakuna biashara wala huduma za kijamii.

“Uharibifu ni mkubwa, sijui nisemeje, na inawezekana kuna polisi karibu watano wameuawa, kwani wananchi nao wana bunduki za magobore wanajibu mapigo. “Jambo la kushangaza ni kwamba, wananchi wengi wanaonekana kuwa na mabomu ya kuulia samaki, sijui wameyatoa wapi. “Wametumia mabomu kubomoa daraja la Mpakula na Mikindani, eneo hili ndilo linaunganisha mikoa ya Mtwara na Lindi, hadi tunavyozungumza hapa hakuna mawasiliano yoyote,” kilisema chanzo chetu. Alisema hali ilianza kuwa mbaya zaidi ilipofika saa 4 asubuhi, ambapo wananchi walianza kujikusanya na kupitapita mitaani, huku wakipishana na polisi.

Chanzo hicho, kinasema katika vurugu hizo, gari la polisi lenye namba za usajili PT 2028 ambalo lilikuwa limebeba maji ya kuwasha, lililipuliwa vibaya na kitu kinachosadikiwa kuwa bomu, baada ya kurushwa na wananchi. “Huwezi amani, lile gari lenye maji ya kuwasha, limelipuliwa vibaya mno, hatujui wananchi wale walitumia kitu gani,” kilisema chanzo chetu.

UCHOMAJI NYUMBA

Habari zinasema kadiri muda ulivyozidi kwenda, makundi ya wananchi walivamia nyumba ya Diwani wa Kata ya Chikongola, aliyetajwa kwa jina moja la Chihako, ofisi za CCM Wilaya ya Mtwara ambazo ziko eneo la Magomeni na nyumba ya mtangazaji wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), Kassim Mikongolo. Pia wananchi hao, walichoma nyumba moja ya kulala wageni ya Shengena Lodge, ambayo inadaiwa kuhifadhi askari polisi, waliokuwa wametolewa mkoani Dar es Salaam. Taarifa hizo, zinasema hali ilikuwa mbaya zaidi katika Mtaa wa Mdenga, ambako wananchi kadhaa wanadaiwa walikuwa wakitumia bunduki aina ya magobore kujibu mapigo dhidi ya polisi.

MATAIRI

Kila kona ya mji wa Mikindani, ilitawaliwa na uchomaji mwingi wa matairi. Kutokana na hali hiyo, polisi na askari wa Kikosi cha Zimamoto, walikuwa na kazi ngumu ya kuzima na kufukuza wananchi.

Source: Mtanzania (May 2013). Vita mtwara. Retrieved from Mtanzania

No comments: