CHAMA cha Wananchi (CUF), kimewataka Watanzania kuhakikisha wanabadilisha mfumo wa maisha kwa kutoipa kura Chama Cha Mapinduzi (CCM), katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015, kwani muda wa ubabaishaji umefikia kikomo. Akizungumza na wananchi wa tarafa ya Pingwe mkoani hapa jana, Mwenyekiti wa chama hicho, Profesa Ibrahim Lipumba alisema kuna mambo mengi ambayo yanachangia hali ngumu ya maisha ya wananchi na moja ya sababu kubwa ni CCM kuendelea kuwepo madarakani, licha ya kushindwa kutatua kero na changamoto zinazowakabili Watanzania. Alisema ni wakati mzuri wananchi kuweka msimamo kuwa ikifika wakati wa uchaguzi wa Serikali za Mitaa mwaka 2014 na uchaguzi mkuu mwaka 2015, CCM haipati nafasi ya kushinda kwenye chaguzi hizo, ili CUF iweze kushika dola.
"Umefika wakati wa kusema ubabaishaji sasa basi, hatuwezi kuendelea kama wananchi mtaendelea kuikumbatia CCM. Ni jinamizi baya ambalo linakwamisha ukuaji wa maendeleo yetu. "Kuendelea kuiacha CCM madarakani, ni kuendelea kubaki masikini, tunajuana Watanzania kila ukienda sehemu watu wamechoka na wamekata tamaa ya maisha. Tumeamua kujipanga kwa ajili ya kuleta mabadiliko na bahati nzuri wananchi wa Tanga na mikoa mingine wanatuamini," alisema Profesa Lipumba.
Alisema maisha ya wananchi, yameendelea kuwa magumu kila kukicha na kutolea mfano huduma za jamii kuwa zimeendelea kuwa duni, hasa maeneo ya vijijini. Kuhusu sekta ya elimu, Profesa Lipumba alisema katika eneo hilo, hali imekuwa mbaya kwani Serikali imeshindwa kutafuta suluhu na sasa sekta hiyo imekosa mwelekeo.
Alisema mkoa huo, umejaliwa kuwa na rasilimali nyingi, ikiwemo zao la mkonge ambalo kwa sasa limekosa msukumo. "Katika soko la dunia, inaonyesha Tanga ilikuwa ikizalisha tani 234,000 kwa mwaka, lakini sasa imeporomoka na kufikia tani 25,000 tu.
Source: Mtanzania (March 2013). Lipumba aitangazia CCM kiama. Retrieved from Mtanzania

No comments:
Post a Comment