Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora

Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora
----------------------WE THANK AND APPRECIATE YOU FOR VISITING CHADEMA DIASPORA BLOG. AGAIN, THANK YOU!-----------------------

Monday, February 10, 2014

Taswira ya Tanzania yachafuka nchini Uingereza kwa ujangili

   Wakati Rais Jakaya Kikwete akijiandaa kwenda London Uingereza kuhudhuria mkutano wa kuokoa viumbe vilivyo hatarini kutoweka duniani ukianza wiki hii, tatizo la ujangili limeweka wingu zito kwa Tanzania. Rais Kikwete ni kati ya viongozi wa nchi 50 watakaohudhuria mkutano huo, utakaokuwa chini ya wenyeji wa mwana wa Wales na Waziri wa Mkuu wa Uinegerza, David Cameron, Taarifa ya gazeti la The Mail on Sunday la Uingereza la Februari 8, limeitaja Tanzania kama kinara wa ujangili kwa kuua zaidi ya tembo 11,000 kwa mwaka, huku Rais wake (Jakaya Kikwete) akielezwa kufumbia macho. Pia, gazeti hilo limemhusisha Rais Kikwete kuwa na urafiki na wafanyabiashara ya meno ya tembo, huku likiwahusisha wafadhili wa Chama cha Mapinduzi (CCM) katika biashara hiyo.
      “Utawala wa Rais Kikwete umetawaliwa na mauaji ya tembo yaliyovunja rekodi katika historia ya nchi yake. Kibaya zaidi, wahifadhi wanasisitiza kuwa, ndani ya Serikali kuna viongozi wanaoshiriki biashara hiyo,” imesema sehemu ya taarifa hiyo. Katika mkutano huo, viongozi wa nchi 50 na mawaziri wataweka mikakati dhidi ya biashara haramu ya wanyamapori, yenye thamani ya pauni 6 bilioni za Uingereza kwa mwaka zinazotumika kufadhili magaidi. Taarifa hiyo inasema kuna wafanyabiashara wakubwa wa Dar es Salaam wanaohusika na ujangili. “Miongoni mwao ni  matajiri wakubwa nchini, wafadhili na wanachama wa CCM na ndugu wa karibu wa Rais Kikwete. Lakini wanao marafiki wakubwa, huku majaji, waendesha mashtaka na polisi hurubuniwa kwa urahisi,” inasema sehemu ya taarifa hiyo.
      Pia, taarifa hiyo inadai kuwapo kwa idadi kubwa ya Wachina wanaofanya biashara ya mafuta nchini, huku baadhi yao wakihusika na ujangili. Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Ikulu, Salva Rweyemamu alikiri kuona taarifa hiyo na kwamba, Rais Kikwete atahudhuria lakini aliipuuza taarifa hiyo. “Ni kweli Rais Kikwete atahudhuria huo mkutano, lakini taarifa ni ya None sense, crap and malicious (ya kishenzi, kipuuzi na ovu),” alisema Rweyemamu. Juhudi za kumpata Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu hazikufanikiwa baada ya simu yake kuita  muda mrefu bila kupokelewa. Hata Naibu wake, Mahmoud Mgimwa naye hakupokea simu alipopigiwa.
       Kuhusu CCM taarifa hiyo imeitaja idara ya wanyapori kunuka rushwa huku ikisingizia kuuzwa kwa meno ya tembo yaliyoko ghalani kwenye soko la kimataifa wakati lengo lao ni kupata fedha kuisaidia chama hicho  uchaguzi mkuu wa mwaka 2015. “ Wabunge, maofisa wa juu na wafanyabiashara, wametajwa bungeni na kwenye vyombo vya habari, lakini uchunguzi unapotezwa,” inaongeza. Jitihada za kupata viongozi wa CCM hazikuzaa matunda.
Mwananchi

No comments: