Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora

Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora
----------------------WE THANK AND APPRECIATE YOU FOR VISITING CHADEMA DIASPORA BLOG. AGAIN, THANK YOU!-----------------------

Saturday, June 8, 2013

Rais marufuku kujihusisha na chama

RASIMU KATIBA MPYA

      KAMA Watanzania wataridhia rasimu ya katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliyozinduliwa wiki iliyopita na Tume ya Mabadiliko ya Katiba bila mabadiliko, itapiga marufuku Rais wa Tanzania kujihusisha kwa namna yoyote na chama chochote cha siasa kikiwemo chama chake, Tanzania Daima Jumapili limebaini. Pendekezo hilo limo katika Ibara ya 69 ya rasimu hiyo inayobainisha madaraka na majukumu ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiwa Mkuu wa Nchi, Kiongozi wa Serikali na Amiri Jeshi Mkuu. Ibara ya 69(4) ya rasimu hiyo inabainisha kuwa: “Katika kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa ibara hii, rais ataepuka kujinasibisha, kwa namna yoyote ile, na chama chochote cha siasa au kundi lolote kwa namna ambayo inaathiri umoja wa wananchi.”

      Katika ibara inayotangulia, ya 68(2) Rais wa Jamhuri ya Muungano ametajwa kuwa atakuwa Mkuu wa Nchi, Kiongozi wa Serikali na Amiri Jeshi Mkuu, na kwa mamlaka hayo kwanza atakuwa alama na taswira ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na watu wake, pili atakuwa alama ya umoja na uhuru wa nchi na mamlaka yake na mwisho atakuwa na dhamana ya kukuza na kuhifadhi umoja wa kitaifa. Lengo la kuwekwa marufuku hiyo limebainishwa wazi na ibara yenyewe kuwa ni kulinda umoja wa wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na umoja wa kitaifa kwa ujumla.

        Kama rasimu hiyo itapitishwa katika kura ya maoni mwakani, rais hataruhusiwa kushiriki katika mikutano ya kawaida ya hadhara, katika mikutano ya kampeni za uchaguzi au shughuli nyingine yoyote ya chama chake, isipokuwa vikao vikuu vya maamuzi vya chama chake. Wachambuzi wa masuala ya siasa wanasema kuwa kama kifungu hicho kitakubaliwa kama kilivyo, litakuwa pigo kubwa kwa chama tawala nchini - Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambacho kimekuwa kikiwatumia wanachama wake ambao ni viongozi wa serikali, akiwemo rais kujinufaisha kisiasa. Kwa muda mrefu tangu kurejeshwa kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa nchini, vyama vya upinzani vimekuwa vikiwalalamikia viongozi wa serikali kutumia nafasi zao serikalini kufanya kazi za siasa za CCM, hususan nyakati za uchaguzi.

         Viongozi wa serikali ambao wamekuwa wakilalamikiwa ni pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muunagno wa Tanzania, mawaziri, wakuu wa mikoa na wakuu wa wilaya ambao wamekuwa wakitumia nafasi zao serikalini kuifanyia kampeni CCM kwa kutumia rasilimali za umma. Aidha, kumekuwepo malalamiko kama hayo dhidi ya marais wastaafu, akiwemo mwasisi na Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere ambaye katika uchaguzi mkuu wa kwanza wa vyama vingi wa mwaka 1995, alisimama kumfanyia kampeni aliyekuwa mgombea urais wa CCM, rais mstaafu Benjamin Mkapa. Kilicholalamikiwa zaidi ni kauli yake kwamba; “siwezi kuiachia nchi yangu ikichukuliwa na mbwa” iliyowakera viongozi wa upinzani kwa kufananishwa na mbwa, hususan aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya Chama cha NCCR-Mageuzi, Augustino Mrema aliyekuwa akipewa nafasi kubwa ya kushinda.
Wachambuzi wa masuala ya siasa wanasema kwa kiasi kikubwa kauli hiyo ya Mwalimu Nyerere iliathiri na kuteteresha heshima yake mbele ya umma wa Watanzania.

Source: Tanzania Daima (June 2013). Rais marufuku kujihusisha na chama. Retrieved from Tanzania Daima

No comments: