Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora

Wasiliana nasi : chademadiaspora@gmail.com -Fair and Balanced Platform- Twitter @ChademaDiaspora
----------------------WE THANK AND APPRECIATE YOU FOR VISITING CHADEMA DIASPORA BLOG. AGAIN, THANK YOU!-----------------------

Thursday, June 6, 2013

CCM inakufa



        MAKAMU Mkuu wa Chuo cha Mtakatifu Augustine (SAUT) kilichoko mkoani Mwanza, Dk. Charles Kitima, ameitaka serikali ya CCM ijiandae kuondoka madarakani kwa aibu hata ikiiba kura.Dk. Kitima alitoa kauli hiyo jana mkoani hapa mbele ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mahusiano na Uratibu, Steven Masatu Wasira, ambapo alisema CCM imeonyesha idhaifu mkubwa katika kusimamia baadhi ya mambo. Wasira na Dk. Kitima walikuwa kwenye mjadala wa Dira ya Maendeleo ya Serikali, uliofanyika mbele ya wanafunzi wa chuo hicho cha SAUT Nyegezi, jijini Mwanza. Dk. Kitima alisema licha ya Wasira kutokuwa fisadi na ni mwanafunzi mzuri wa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, alimtaka awaambie wenzake wajiandae kuondoka kwa aibu.

       “Mfano mzuri, Singapore wao walianza kusimamia utalii, lakini serikali yetu ilikosea sana kutokutekeleza mambo ya uzalishaji. Na msipotekeleza hili, CCM mtaondoka madarakani.“Ulaji mkubwa wa fedha umeingia sekta ya elimu, hamtekelezi kwa vitendo sera na dira za taifa. Nasema msipobadilika serikali ya CCM itaondoka na hata mkiiba kura, lazima mtaondoka tu, tunawaandalia wapinzani,” alisema Dk. Kitima kisha ukumbi mzima ukamshangilia kwa nguvu. Dk. Kitima ambaye kitaaluma ni mwanasheria, alisema Rais Jakaya Kikwete anao mawaziri watatu tu ambao wana mrengo chanya wa kuikomboa nchi. Alibainisha kuwa kitendo cha serikali kuruhusu wawekezaji kuingia nchini na kudharau wazawa na mali zao hilo litakiangusha chama tawala.

        Alisema kwa sasa katika vikao vya Bunge, hoja za msingi zinapingwa huku mtoa hoja akizomewa, lakini mambo ya kipuuzi ndiyo yanayoshabikiwa na wabunge wengi. Naye Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mahusiano na Uratibu, Steven Masatu Wasira, amewashukia watumishi wote wanaojihusisha na ubadhirifu wa mali za nchi na kusema lazima watu hao wahenyeshwe kwa kuchukuliwa hatua bila kuonewa aibu. Wasira ambaye ndiye aliyekuwa mgeni rasmi, alianza kwa kusema: “Mimi nachukizwa sana na wanaoiba mali za nchi. Sipendi wizi na siwezi kuiba wala simung’unyi maneno kusema hili.” Alisema wapo baadhi ya watumishi wanapoingia kwenye ajira kazi yao ni kuanza kuiba badala ya kujenga taifa, jambo ambalo ni hatari kwa maendeleo ya nchi, na kwamba fedha za EPA zilizorudishwa na wezi na zimetumika kuinua kilimo.

           Waziri Wasira alisema kupungua kwa uadilifu hapa nchini ni tatizo kubwa, na linaweza kuleta mgogoro mkubwa na kudidimiza zaidi uchumi wa nchi, hivyo lazima kila Mtanzania awe muumini mzuri wa uzalendo. “Rasilimali zote za nchi lazima zitumike kuwanufaisha Watanzania wote. Na bila hivyo hakuna nchi. “Kupungua kwa uzalendo na uadilifu ni tatizo kubwa sana kwa nchi. Lazima tuenzi amani na upendo...ukishindwa kulinda na kuiheshimu Tanzania wakati na wewe ni Mtanzania hufai,” alisema Wasira. Alisema rasilimali zote yakiwemo madini, maziwa, utalii na nyinginezo nyingi ni vema zikageuzwa kuwa mali zinazonufaisha na kuleta maendeleo kwa wananchi na kwamba dira ya maendeleo ya taifa ni kuboresha fursa nyingi za kiuchumi.

          Alisema ili kufikia malengo halisi, mpango wa serikali uliopo sasa ni kuboresha huduma za viwanda, reli, viwanja vya ndege, kilimo bora, bandari, maliasili, miundombinu na nishati.Kuhusu udini, Wasira alisema wamemeishi miaka 50 kwa amani, upendo na utulivu lakini sasa kuna chokochoko za baadhi ya watu ambao hawataki kuiona nchi ikitulia.Aliwataka wasomi, waandishi wa habari, wanasiasa, viongozi na waumini wa dini zote na makundi ya kijamii, kuhakikisha wanapigania kuendelea kumea zaidi uharibifu wa amani ya nchi, maana lazima kila Mtanzania aihurumie nchi.

Source: Tuma S. (June 2013) CCM inakufa. Mwanza. Retrieved from Tanzania Daima

No comments: